Monday, September 13, 2010

GAZETI LA LEO - MPANDA

NKASI - WAMPEMBE - 17 MBARONI KWA KUVAMIA KITUO CHA POLISI
WATU kumi na saba wanashikiliwa na jeshi la polisi mkoani Rukwa kwa tuhuma za kuvamia kituo cha polisi kwa lengo la kutaka kukiteketeza kituo hicho kwa moto.
Kamanda wa polisi mkoani Rukwa Isuto Mantage amesema Novemba 30,2010 ofisini kwake kuwa wanaoshikiliwa ni wanakijiji wa kijiji cha Wampembe wilaya ya Nkasi mkoani Rukwa baada ya jaribio la kutaka kukitekeza kwa moto kituo kidogo cha polisi cha Wampembe kwa lengo la kumuua mtu mmoja waliyekuwa wanadai kuwa ni mchawi.
Amesema kuwa awali katika kijiji hicho kulitokea msiba wa kijana aliyetajwa kwa jina la Joseph Kapelo (19) baada ya kuugua muda mfupi mnamo Novemba 22, 2010 ambapo kijana huyo aligua majira ya saa mbili asubuhi nakufariki saa tano mchana kifo kilichozua mijadala kijijini hapo wakazi wengi wakidai kuwa marehemu alikuwa amefariki kutokana na imani za kishirikina.
Amefafanua kuwa baada ya kupata taarifa za kifo hicho wananchi walianza kukusanyika katika msiba na kuanza kupanga mikakati ya kummaliza baba wa marehemu aliyetajwa kwa jina la ndugu Daudi Kapelo (76) kwa madai kuwa ndiye aliyamuua mwanae huyo kwani ni miezi miwili tu tangu kijana mwingine mtoto wa huyo mzee alifariki katika mazingira ya kutatanisha kama ilivyotokea katika huo msiba.
Amesema kuwa wakati wananchi hao wakipanga mikakati hiyo taarifa zilifika kituo kidogo cha polisi Wampembe ambapo polisi wa kituo hicho waliweza kuchukua hatua ya kumuokoa Mzee huyo lakini kabla hawajafika msibani tayari Mzee huyo alikuwa ameshaanza kushambuliwa na wananchi na kuokolewa na polisi na mgambo na kasha kuchukuliwa na kwenda kuhifadhiwa kituo cha polisi kwa usalama wake.
Amesema wakati wananchi hai wakielekea kuzika walichukua jeneza la marehemu na kwenda nalo hadi kituo cha polisi ambapo waliliweka jeneza hilo hapo kituoni na kudai wanataka Mzee Daudi Kapelo atolewe humo ndani wammalize naye akazikwe na mwanae na kuanza kushambulia kituo hicho kwa mawe hali iliyopelekea askari kupiga risasi hewani lakini wananchi hao hawakuweza kuogopa na kuanza kumshambulia askari huyo na kuibua mapigano baina ya askari na wananchi wapatao 300.
Amesema kuwa wananchi hao baada ya kutawanyika walikimbia wote wakiwa tayari wameshawasha moto kituo cha polisi kikiungua ambapo askari polisi na mgambo kwa kusaidiana na viongozi wa kijiji walifanikiwa kuuzima moto huo na wananchi hao waliweza kurudi usiku wakachukua maiti ya merehemu na kwenda kuzika usiku huo huo.
Amesema mapambano hayo yaliendelea ambapo mwananchi mmoja Imelda Kayanda (46) alipigwa risasi na kufariki na Agnes Kisori(21) alijeruhiwa mguuni huku vitu vilivyoharibiwa vikiwa ni pamoja na solar panel ya kituo, vioo vya kituo vyote kwa pamoja vikiwa na thamani ya shilingi laki tano.
Amesema majeruhi walipelekwa kituo cha afya Wampembe na baadae hospitali ya wilaya ya Nkasi kupata matibabu ambapo hali zao zimeelezewa kuwa zinaendelea vema.
Amesema tayari jeshi la polisi limewakamata ndugu Zakaria Francis (28), Ikombe Yustini (39), Stephano Kambe (18), Benard Kabeja (16) na John Kapandila (22).
Wengine waliokamatwa amewataja kuwa ni ndugu Said Diwali (36), Vido Tuwakazi (21), Abdalah Vicent (19), Sylveter Kapala (17), Richad Bushota (19), John Mathias (58), Wilbroad Chambi (16) na Kapondo Anatoli (23) na wengine wane wote wakazi wa kijiji cha Wampembe wilaya ya Nkasi.
Kamanda wa Polisi amesema wakati watuhumiwa hao wote watafikishwa mahakamani mara baada ya upelelezi kukamilika na kuwa wengine waliokimbia watafuatiliwa hadi wakamatwe ili sheria ichukue mkondo wake.
Aidha kamanda Mantage ametoa wito kwa wananchi kuacha tabia ya kujichukulia sheria mkononi na tabia mbaya ya kuvamia vituo vya polisi nchini hapa nchini kuwa vinalipeleka taifa kusikojulikana kutokana na ukweli kuwa hizo ni dalili za kuondoa misingi ya amani na utulivu katika jamii.
MWISHO
MBUNGE mmoja wa Chama Cha Mapinduzi wilayani Mpanda amelalamikiwa kuwafanyia kitu mbaya vijana watatu akiwemo mlemavu asiyekuwa na uwezo wa kutembea.
Taarifa zilizolifikia gazeti hili zimeeleza kuwa mbunge huyo mwenye sifa ya kuitwa Mbuyu mdogo amewadhulumu vijana watatu waliokuwa watumishi wa ofisi yake ya bunge katika jimbo lake ofisi zilizoko mjini Mpanda baada ya kuwatumikisha bila kuwalipa mishahara yao halali.
Wakiongea kwa uchungu vijana hao pamoja na binti mmoja mlemavu wa miguu aisyeweza kutembea kwa miguu ya kawaida walidai kuwa mbunge huyo amewadhulumu zaidi ya shilingi miliono moja na laki nane zikiwa ni mishahara na posho za kazi zaidi ya shilingi milioni moja na laki mbili.
Kijana mmoja aliyejitambulisha kwa jina la Peter Pulwila Panta aliyekuwa ameajiriwa kwa kazi ya udereva na kupewa kitambulisho chenye nambari 001 alisema wamekuwa wakimdai mbunge huyo mishahara yao lakini cha kusikitisha amekuwa akidai kuwa hizo pesa hajaletewa kutoka ofisi ya bunge kitu ambacho si kweli kutokana na maelezo yaliyoko katika barua yenye kumb namba FA.155/2006/01/70.
Alisema licha ya kuwa barua inaagiza kuwalipa mshahara wa kiasi cha shilingi 150,000 kwa mwezi lakini yeye aliwaeleza kuwa watakuwa wanalipwa shilingi laki moja kila mwezi na kuwa alikuwa anakidai kuwa anawalipa kutokana na mshahara wake wa ubunge ihali barua inaonesha kuwa fedha hizo zinatumwa kila mwezi katika akaunti ya mbunge huyo kwa ajili ya mishahara na posho.
Naye binti mwenye ulemavu aliyekuwa akifanya kazi kama mhudumu wa ofisi ya mbunge huyo alisema kuwa tangu mwaka 2005 alikuwa akifanya kazi na kupewa hela ya soda tu shilingi 20,000/= tu kila anapodai mshara wake na kuwa ukosefu wa mshahara kumepelekea mwanaye anayesoma katika shule ya sekondari Mwese kuzuia kuendelea masomo kutokana na madeni ya ada.
Alipofuatwa na mwandishi wa habari ofisini kwake kujua kulikoni anadaiwa na watumishi wake akiwemo mlemavu wa miguu lakini mbunge huyo hakuweza kupatikana badala yake alikuwepo mtu aliyejieleza kuwa ni katibu wa mbunge huyo ingawa alikataa ktaja jina lake aliyeeleza kuwa mbunge wake yuko katika kikao CCM
Juhudi za kumtafuta kwa simu mbunge huyo zilifanikiwa ambapo mbunge huyo alijibu katika simu kuwa anahitaji kuonana na mwandishi wa habari.
Cha kushangaza ni kuwa alikwenda mwandishi ofisini kwake kuzungumzia suala la madeni na kuzomewa alikozomewa wakati wa mkutano wa hadhara katika kijiji kimoja mbunge huyo alimsihi mwandishi huyo asiandike taarifa yoyote mbaya kumhusu na kumpatia kiasi cha shilingi elfu ishirini kwa ajili ya kumziba mdomo pesa ambazo mwandishi alizikataa na kuondoka
Uchunguzi umebaini kuwa madai hayo na mengine mengi yalishawahi kufikishwa katika ofisi za CCM wilaya ya Mpanda na kukosa suluhu ambapo mbunge huyo amekuwa akijinadi kuwa ni mtaalamu wa propaganda, mbuyu mdogo anataka kugombea mwakani kutetea kiti cha ubunge hivyo wasimjadili kuhusu madeni yake.
Mbunge huyo alijikuta akitemwa katika kura ya maoni ndani ya chama chake katika uchaguzi mkuu wa 2010 nchini Tanzania
MWISHO

MILIONI KUMI HIZI ZIMETUMIKA KWELI NAMNA HII
ZAIDI ya shilingi milini 10.1 zimetumika kwa ajili ya kuwanunulia sare za shule na kuwalipia ada na chakula watoto yatima na wanaoishi katika mazingira magumu wilaya ya Mpanda mkoani Rukwa
Mratibu wa asasi isiyokuwa ya kiserikali ya SHDEPHA + tawi la Mpanda Mwalimu Euzebius Ngulusha alisema hayo jana (Novemba 3, 2009) wakati wa hafla fupi ya kuwakabidhi sare, chakula na mahitaji ya shuleni watoto yatima na wanaoishi katika mazingira hatarishi wapatao 54 iliyofanyika katika ukumbi wa SHDEPHA + mjini Mpanda.
Alisema katika kipindi cha Januari hadi Oktoba mwaka huu zaidi ya shilingi milini 10.1 zimetumika kuwahudumia watoto 204 wanaoishi katika mazingira hatarishi, yatima na watoto wanaoishi na Virusi vya UKIMWI wilayani Mpanda fedha ambazo zimetoka kwa wafadhili mbalimbali ikiwa ni pamoja na shirika la Kimarekani la WALTER REED la nchini Marekani.
Alisema shirika lake limelipia ada za sekondari na kuwanunulia sare za shule watoto wanaosoma katika shule za sekondari wapatao 150 kwa gharama ya shilingi 8,304,300/= na watoto wanaosoma shule za Msingi wapatao 35 na wachache wanaotoka katika mazingira hatarishi.
Alisema kiasi cha shilingi 1,800,000 zimetumika kuwanunulia mahitaji ya shuleni kama vile daftari, kalamu, vihifadhio, mifuko ya shule na vifaa vya kuchorea vya wanafunzi hao ili nao wajisikie kama sehemu ya jamii.
Akiongea kwa niaba ya Mkurugenzi wa Mji wa Mpanda afisaelimu wa sekondari wa Halmashauri ya Mji wa Mpanda Said Mwapongo aliwashukuru viongozi wa asasi hiyo ya SHDEPHA + kwa kufanya kazi ya kuwasaidia wanaohitaji katika jamii na kuvishinda vishawishi wanavyokumbana navyo vishawishi ambavyo amesema vinawapelekea kushikwa na tamaa ya kutumia fedha hizo bila kujali ni za nani.
Alisema moyo wa kuwafikishia walengwa ambao hawakujua kama wanaletewa nini ni moyo wa kipekee na wa kiungwana ambapo amewasihi kutokukata tamaa na kuwa Mungu peke yake ndiye atakayewalipa kwa kazi njema hiyo.
Mwapongo aliwasihi wanafunzi hao kuitumia misaada waliyoipata na wanayoendelea kuipata kwa kusoma kwa bidii, kuwa na heshima katika jamii ili kuwawezesha kufikia malengo yao ambayo ni kuwaondoa katika lindi la maisha ya masikitiko na umasikini uliopindukia.
MWISHO

WANANCHI HAWA WAMECHUKIA DILI ZA POLISI AU NI HASIRA KWELI?
WANANCHI wenye hasira wamefanikiwa kuliua jambazi lililokuwa likitafutwa na jeshi la polisi mkoani Rukwa baada ya kumkuta akiiba magunia ya mpunga
Akiyeuwawa ametajwa kwa jina la Revocatus Benedicto Katunga mwenye umri wa miaka 33 mkazi wa Nsemulwa mjini mpanda ambaye aliuwawa na wananchi Septemba 23,2009 saa kumi na mbili asubuhi mara baada ya kukutwa akiiba magunia ya mpunga katika mashine ya kusaga ya mfanyabiashara anayejulikana kwa jina la Kasimu lyanga maarufu kwa jina la Usayi.
Kamanda wa polisi mkoani Rukwa Isuto Mantage aliwaeleza waandishi wa habari kuwa siku ya tukio marehemu anayesadikiwa kuwa ni jambazi sugu aliyekuwa anatafutwa na jeshi hilo alikutwa na wananchi akiwa katika harakati za kuiba magunia ya mpunga ambapo alikuwa ameshaiba magunia manne ya kuyatoa nje ya jingo hilo .
Alisema baada ya kumkuta marehemu huyo wananchi hao walianza kumhoji lakini akawa anawajibu maneno ya jeuri kwa sauti kubwa iliyowaamusha majirani wengine waliofika hapo na kumkuta jambazi huyo aliyekuwa akitafutwa na jeshi la polisi mkoani Rukwa kwa tuhuma za kushiriki katika matukio kadhaa ya uhalifu walianza kumpa kipigo hadi akapoteza fahamu ndipo wakawaita polisi kituo cha Mpanda.
Alisema kamanda Mantage kuwa polisi walipofika eneo la tukio walimchukua marehemu na kumwahisha hospitali ambako kabla ya kupewa huduma yoyote alifariki akiwa eneo la hospitali.
Kamanda alisema hakuna aliyekamatwa kuhusiana na tukio hilo ambapo alieleza kuwa marehemu alikuwa akitafutwa kwa kosa la kuvunja na kuiba vitabu katika shule ya msingi Katavi iliyoko mjini Mpanda na pia alikuwa na kesi mahakani ya kuiba kwa kutumia silaha
Kwa upande wao wananchi wa eneo la Mpanda Hoteli mjini Mpanda walionesha kusikitishwa kwao na mwenendo wa utendaji kazi wa jeshi la polisi wilayani Mpanda kwani jambazi huyo alikuwa ameshikana kukamatwa na jeshi hilo hadi walipomkamata wananchi wenyewe na kumpa hukumu ya kifo licha ya kuwa alikuwa na matukio mengi ya kutafutwa.
the end

Sunday, August 22, 2010

CHAKACHUA YA PINDA YAISUMBUA CHADEMA

Na Willy Sumia, Mpanda
WAZIRI mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mizengo Pinda ambaye amepita bila kupingwa katika kinyang’anyiro cha ubunge katika jimbo la Katavi mkoa wa Katavi kumeelezewa na wananchi wa jimbo lake kuwa ni uamuzi wa siku nyingi kabla hajateuliwa kuwa Waziri Mkuu.
Hayo yalielezwa na baadhi ya wananchi wa jimbo hilo katika mahojiano ya hivi karibuni na waandishi wa Habari mara baada ya tume ya uchaguzi jimbo la Katavi kutangaza kuwa Pinda amepita bila kupingwa kutokana na wagombea wane wa CUF, CHADEMA, NLD na CHADEMA kujitoa katika kinyang’anyiro hicho kwa barua.
Wananchi hao wanaotoka katika vijiji vya Ilunde, Ilela, Majimoto, Kasansa na Kilida walidai kuwa tangu Pinda awe mbunge wa jimbo lao lililokuwa awali likiitwa jimbo la Mpanda Mashariki kumekuwa na maendeleo makubwa pamoja na mabadiliko ya kiuchumi kwa wananchi hao.
Ndugu Hussein Omari mkazi wa kijiji cha Inyonga alisema kuwa wananchi wa tarafa ya Inyonga walikuwa wakiteseka sana kutokana na kukosekana kwa barabara ya uhakika na mawasiliano ya simu lakini tangu Pinda awe mbunge wao wameweza kupata miundombinu hiyo kwa kasi ya ajabu.
Mmoja wa wagombea waliokuwa wametangaza nia ya kugombea katika jimbo hilo ndugu Sebastiani Kasinge alisema kuwa mara baada ya kuchukua fomu ya kugombea ubunge jimbo la Katavi kwa Pinda alipata upinzani mkubwa sana toka kwa wananchi wa jimbo hilo, ndugu zake na hata ndani ya Chama chake cha CHADEMA.
Alisema kuwa uamuzi wake wa kuchukua fomukatika jimbo hilo ulipelekea mvutano mkubwa ndani ya CHADEMA na kupelekea mbunge wa jimbo la Mpanda kati CHADEMA Said Arfi kutangaza kujitoa katika uchaguzi iwapo chama chake kingesimamisha mgombea jimbo la Pinda ambapo mwenyekiti wa CHADEMA mwasisi aliamua kujivua uanachama wa CHADEMA na kuhamia chama kingine cha siasa katika kikao kilichokuwa kikijadili wagombea.
Chanzo cha uhakika cha habari toka katika chama cha CHADEMA kimeeleza kuwa CHADEMA ndio waliokuwa wakishinikiza Pinda apite bila kupingwa katika jimbo hilo lakini baadhi ya viongozi wa CCM walikuwa wakitaka kuwepo na mgombea ili wapate mshiko wa kampeni katika jimbo hilo na kutofautiana na katibu wa CCM wa wilaya Mohamed Omary Nyawenga aliyeonekana akifanya juhudi za kweli kuhakikisha Pinda anapita bila kupingwa akishirikiana na baadhi ya wananchi wa Inyonga.
MWISHO

Nguruwe kunywa dawa za Kupunguza makali ya VVU ARVs inakuwajeeeeeee

Iringa
WADAU wa asasi zisizo za kiserikali nchini wametoa onyo kwa wafugaji na wakulima wanaotumia dawa za binadamu kuwapa mifugo na kupulizia kwenye mazao na kusababisha ongezeko la madhara makubwa kwa jamii.
Hayo yalizungumzwa na washiriki wa mafunzo ya uchambuzi wa Sera yaliyoandaliwa na Mwamvuli wa asasi za kiraia mkaoni Iringa na Njombe Iringa Civil Society Organizations (ICISO) katika ukumbi wa Lutherani
mjini Makambako katika mkoa mpya wa Njombe wiki iliyopita.
Wadau hao walisema kuwa tabia iliyoibuka hivi karibuni kwa baadhi ya wafugaji na wakulima kutumia dawa zitumikazo kwa ajili ya binadamu kwa kuipa Mifugo hali inayopelekea kuibuka kwa magonjwa yasiyofahamika na kusababisha madhara kwa walaji wa bidhaa zitokanazo na mifugo.
Bwana Obothe Msemakweli mmoja wa wadau kutoka asasi ya LUCAPOA ya wilayani Ludewa alisema baadhi ya wakulima wa zao la nyanya wamekuwa wakipulizia dawa ya kuua Mbu aina ya Ngao katika zao hilo kwa lengo la kuua wadudu waharibifu wa zao hilo hali inayowaletea madhara walaji.
“Unajua wakulima wanapotosha sana matumizi sahihi ya dawa ya Ngao, imefikia baadhi ya wakulima wanapulizia katika miche ya nyanya hali inayopelekea walaji kudhulika,” Alisema Msemakweli.
Walisema pia dawa za uzazi wa mpango ambazo hutumiwa na akinamama kupanga uzazi zimekuwa zikitumiwa na baadhi ya wafugaji huwapa kuku kwa lengo la kuwafanya wakue haraka ili kupata bei nzuri ya mifugo hiyo kutokana na tamaa ya pesa.
Wadau hao walisema wanyama aina ya Nguruwe nao wamekuwa wakipatiwa vidonge vya ARVs ambavyo hutolewa kwa wagonjwa wa Ukimwi ili kuwaongezea siku za kuishi na mazao ya mahindi na Maharage yamekuwa yakiwekewa dawa ya Ngao ya unga kwa imani kuwa hayatabunguliwa na Fukuzi wadudu waharibifu wa mazao.
Bi Grace Sanga wa asasi ya PROMISE ya mjini Iringa alisema upotoshwaji wa matumizi hayo ya dawa yanajengwa na uzushi ambapo wafugaji na wakulima huamini kuwa baada ya kuwapa mifugo dawa za binadamu, kuku na Nguruwe hukua haraka bila kuwa na ushauri wa kitaalamu.
Bwana Renatus Mpiluka mwanachama wa asasi ya MUNGONET ya Mufindi alifafanua kuwa hali hiyo inatokana na sera nyingi kutungwa na kuishia katika vitabu na wananchi kushindwa kuzifahamu hali inayopelekea baadhi ya wananchi kufanya mambo kinyume na utaratibu wa sera husika.
“Sera ya Kilimo, yenye kauli mbiu ya Kilimo kwanza naieleweki kwa baadhi ya wakulima ambao ndiyo walengwa wakuu wa mpango huo, kuna hajaya serikali kutoa elimu sahihi ya sera ili jamii izifahamu.” Alisema
Renatusi
Naye ndugu Leonard Kalolo mujumbe wa asasi ya LIMAU ya Mgololo wilayani Mufindi alisema wakulima na wafugaji wapatiwe elimu ili kupunguza matumizi yasiyo sahihi ya dawa hizo pamoja na udhibiti wa usambaaji wa dawa za binadamu.
“Mbolea na madawa zinatumiwa vibaya, unakuta mtu anaweka mbolea hata kwenye mazao ya muda mfupi kama mboga mboga, hii inasababisha kumfikia mlaji kemikali za madawa hayo zikiwa bado hazijaisha na
kusababisha maradhi ,” alisema ndugu Kalolo.
Wadau hao wa asasi zisizo za Serikali waliitaka serikali itoe elimu sahihi kwa wakulima juu ya Sera mbalimbali zitolewazo na serikali ikiwa ni pamoja na kuwashirikisha wananchi katika utungaji wa Sera
kwani wao ndiyo watekelezaji wakuu wa irani hizo.
Naye muhadhiri wa chuo kikuu cha Tumaini mkoani Iringa Lucas Mwahombela aliitaka serikali kuingilia kati ukiukwaji wa matumizi hayo ikiwa ni pamoja na kuziweka wazi sera mbalimbali hasa za Kilimo ambazo
zinawalenga watu wa hali ya chini ili wazielewe na kufanikisha sera ya Kilimo kwanza na kauli mbiu ya Mapinduzi ya Kijani.

MWISHO
Na Willy Sumia, Mpanda
MWENYEKITI mwasisi wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo wilaya ya Mpanda mkoa wa Rukwa amekihama chama chake baada ya kunyimwa fursa ya kuwa mgombea wa Udiwani katika kata mpya ya Makanyagio mjini Mpanda katika mkoa wa Katavi.
Mwenyekiti huyo Bwana Juma Mausi alihama chama chake mara baada ya kuanza kwa mchakato wa uchaguzi mkuu wa 2010 kuanza kupamba moto kufuatia kuanza kwa mikutano ya kampeni na kujikuta akitupwa nje ya timu ya wagombea wa CHADEMA katika kinyang’anyiro cha udiwani kata ya Makanyagio baada ya nafasi hiyo kupewa mjumbe wa serikali ya mtaa wa Kachoma ndugu Nziguye Juma.
Juma Mausi ambaye ndiye aliyeipokea na kuasisi chama cha CHADEMA wilaya ya Mpanda wakati wa vuguvugu la vyama vingi nchini alijikuta akikihama chama chake baada ya kubaini kile alichokieleza yeye
mwenyewe kuwa CHADEMA imekamatwa na wageni na kukiita kitendo hicho kuwa ni Uvamizi wa kisiasa ndani ya CHADEMA yake.
Taarifa sahihi toka katika chanzo cha kuaminika ndani ya CHADEMA zimeeleza kuwa baada ya kuona haridhishwi na uamuzi aliofanyiwa ndani ya CHADEMA Mzee Mausi aliamua kujiunga na chama cha NCCR Mageuzi ambako alipewa nafasi ya kuwa mgombea wa chama hicho katika king’anyiro cha udiwani kata ya Makanyagio ili kupambana na wagombea wa CCM, CHADEMA na CUF.
Juma Mausi alikuwa mwenyekiti wa CHADEMA wilaya ya Mpanda hadi Agosti alipotangaza kuachana na chama hicho na kuhamia NCCR Mageuzi hali iliyopelekea CHADEMA wilaya ya Mpanda kutafuta mwenyekiti wa muda katika kipindi hiki cha uchaguzi ambapo chama hicho kinatetea nafasi ya ubunge jimbo la Mpanda mjini ambapo mbunge wa sasa wa jimbo hilo ni mheshimiwa Said Arfi wa CHADEMA.

mwisho

Saturday, August 14, 2010

BARABARA ZA LAMI RUKWA

RAIS Jakaya Mrisho Kikwete amewka jiwe la Misngi katika mradi mkubwa
wa umeme wenye thamani ya shili Bilioni 12 kwa ajili ya Miji ya
Namanyere na Sumbawanga mkani Rukwa. Mradi huo uliwekewa jiwe la msingi katika eneo la Mitambo ya umeme ya shirika la umeme nchini TANESCO mjini Sumbawanga Jumamosi iliyopita unajumuisha mashine nne kubwa zenye uwezo wa kuzalisha kilowatt 5 za umeme kwa wakati mmoja zilizonunuliwa na serikali kwa gharama ya shilingi Bilioni 3.
Akitoa taarifa mbele ya Mheshimiwa Rais Waziri wa Nishati na Madini Wiliamu Ngeleja alisema kuwa mradi huo wa umeme unaanza Julai 2010 na kukamilika Juni 2011 ambapo waziri huyo alimueleza rais kuwa umeme utaanza kuwaka mjini Namanyere Machi 2011. Aidha Waziri Ngeleja alisema kuwa mradi huo utawawezesha wananchi waishio katika vijiji vinavyopitiwa na nguzo za umeme katika barabara ya kuelekea Namanyere mjini kupatiwa umeme kwa ajili ya matumizi ya majumbani na matumizi mengine kama ilivyo kwa wananchi wa mijini.Waziri Ngeleja alisema kuwa Serikali imeondoa gharama za nguzo kwa wananchi wa vijijini ili kupunguza gharama za kuingiza umeme katika nyumba zao na badala yake gharama za nguzo zitakzotumika kuingizia umeme kwa wananchi serikali ndiyo itakayogharamia kutokana na ukweli kuwa wananchi wa vijijini wana kipato kidogo ukilinganisha na waishio mijini.
Naye Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dr. Jakaya Mrisho Kikwete aliwataka wananchi wa vijiji husika kuanza kujiandaa kuupokea umeme pindi utakapofika ikiwa ni pamoja na kuachana na ujenzi wa nyumba za nyasi kwa rais alisema nyasi hazipatani na umeme “ Ndugu zangu wananchi wa Kipande na wengine walioko katika njia hii, changamkieni umeme huu ili mpate maendeleo ya haraka, acheni kujenga nyumba za nyasi kwa sababu umeme na nyasi haviendani, jengeni nyumba bora hivi sasa ili umeme ukifika kijijini kwenu muupokee na kuanza kuufaidi” alisema Mhe. Rais Rais Kikwete alisema hivi sasa wananchi wa Rukwa neema imewashukia kwani tayari umeme wanatarajia kuupata wa uhakika, barabara nazo zinajengwa kwa kiwango cha lami na pia kuna maboresho ya kilimo kupitia dhana ya KILIMO KWANZA.
Alifafanua kuwa kilimo kikizalisha mazao ya kutosha sasa wananchiwataweza kusafirisha mazao hadi kwenye soko bila matatizo na tena wakiuza mazao kwa bei nzuri katika soko wataweza kuutumia umeme
kujiletea maendeleo na hayo ndo maisha bora kwa kila Mtanzania.

MWISHO

ACHENI USHOGA NA WATENDAJI-JK

MADIWANI wametakiwa kuacha kuwa marafiki wa watendaji na wakurugenzi wa Halmashauri zao ili kuweza kudhibiti vitendo vya ufujaji wa pesa za serikali zinazoletwa katika maeneo yao kwa ajili ya shughuli za maendeleo.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dr. Jakaya Mrisho Kikwete alipokuwa akihutubia wananchi katika mkutano wa hadhara mjini Mpanda katika Ziara yake Mkoani Rukwa . Rais Kikwete alisema kuwa hivi sasa kumekuwa na ufujaji mkubwa wa fedha za serikali hasa zinazoletwa na serikali kuu kama ruzuku ya
maendeleo katika halmashauri mbalimbali nchini lakini zimekuwa hazioneshi kuleta mabadiliko katika jamii husika. Alisema tatizo la ubadhilifu wa fedha za wananchi kwa ajili ya kuwaletea maendeleo wananchi limekuwa likiongezeka siku hadi siku na hali inakuwa mbaya zaidi katika maeneo ambayo madiwani wamekuwa na urafiki na ushoga na watendaji wa halmashauri na wakurugenzi wa maendeleo. “ Hizi pesa wanaotakiwa kuzisimamia na kuhakikisha zinafanikisha malengo yaliyokusudiwa ni madiwani lakini kwa bahati mbaya madiwani katika maeneo mengine wamekuwa wakijenga urafiki na ushoga na
watendaji wa halmashauri na wakurugenzi ambao ni wezi wao, wanaishia kupewa gawio kidogo wanaridhika na kuona mambo safi kumbe wanaibiwa maana pesa za ruku ya maendeleo ni ya wananchi na wadhamini wao ni madiwani” alisema Rais Kikwete Rais Kikwete alisema madiwani wanatakiwa kuelewa kuwa wao wana dhamanaya wananchi kuwasimamia wakuu wa idara na waandamizi wao katika vikao na nje ya vikao na ikiwezekana wachukue hatua pale wanapobaini kuwepo kwa hujuma katika pesa zao bila kusita badala ya kuiachia serikali peke yake.
“Kimsingi pesa zinzoletwa na serikali kuu kama ruzuku ya maendeleo ni za wananchi na wala si za serikali ndiyo maana sisi tunawaletea huku kwenye halmashauri zenu ili zijenge barabara, madarasa, zahanati, miundombinu ya maji na Miradi mingine ya maendeleo ya wananchi ambao ninyi madiwani ni wawakilishi wao, acheni urafiki na ushoga na watendaji na wakurugenzi wa Halmashauri zenu, wasimamieni.” Alisisitiza Rais Kikwete Aidha mkuu wa mkoa wa Rukwa alimshukuru Rais Kikwete kwa serikali yake
kuhakikisha inaondoa kero kubwa kwa wananchi wa mkoa huo ya barabara zisizo pitika mwaka mzima na kuamua kujenga kwa kiwango cha lami kuwa huo ni ukombozi mkubwa kwa wananchi wa Rukwa.

MWISHO

Monday, June 21, 2010

HASIRA ZA MKIZI!!!!!!

MWALIMU AMTWANGA RISASI MKEWE
MWALIMU wa shule ya msingi Safu kata ya Katete Tarafa ya Matai wilaya ya Kalambo mkoani Rukwa anasakwa na jeshi la polisi mkoani Rukwa kwa tuhuma za kumjeruhi mke wake kwa risasi kufuatia ugomvi baina yao.
Kamanda wa Polisi mkoa wa Rukwa Isuto Mantage amesema mbele ya waandishi wa habari jana kuwa tukio hilo lilitokea juzi Agosti 25,2010 majira ya saa kumi alfajiri katika kijiji hicho ambapo mwalimu Patrick
Edward (40) wa shule ya Msingi Safu alimjeruhi kwa risasi sehemu za tumboni na kiunoni mke wake Bi Agnes Mwingira (35) ambaye pia ni mwalimu wa shule hiyo.
Kamanda Mantege amesema kuwa mnamo Agosti 24,2010 majira ya asubuhi kuliibuka ugmvi baina ya mwalimu huyo na mkewe kutokana na mkewe kumtuhumu mumewe kuwa mwalimu huyo alikuwa na uhusiano wa kimapenzi na mfanyakazi wao wa ndani.
Amesema wanandoa hao walisuluhishwa na majirani na kuyamaliza lakini muda wa alfajiri ya saa kumi ya agosti 25, 2010 ugomvi ulizuka tena yao hali iliyopelekea mwalimu huyo kumfyatulia risasi mkewe kiunoni na tumboni kwa kutumia bunduki aina ya short gun inayomilikiwa kihalali na mwalimu huyo.
Imeelezwa kuwa mwalimu huyo alipomaliza kufanya unyama huyo huku akidhani kuwa ameshamuua mkewe alichukua bunduki hiyo na kutokomea kusikojulikana pamoja na bunduki hiyo.
Majirani walipofika katika nyumba hiyo baada ya kusikia milio ya bunduki walimkuta mke wa Mwalimu Bi Agness Mwingira akitokwa damu nyingi tumboni na kiunoni bila msaada wowote ndipo walimchukua majeruhi na kumsafirisha hadi katika hospitali ya mkoa wa Rukwa kwa ambapo hali yake imeelezwa kuwa ni mbaya.
Kamanda wa polisi amesema kuwa jeshi la polisi linawahoji watu mbalimbali kijijini hapo ili kujua chanzo hasa cha matumizi ya risasi kwa mkewe huyo ambapo miongoni mwa wanaohojiwa ni pamoja na mwalimu
mkuu, mjomba wanayeishi naye, mtumishi wa ndani pamoja na majirani.
MWISHO.