Sunday, November 4, 2012

HABARI ZA MKOA WA KATAVI



MTAA WA FISI MJINI MPANDA KAAAZI KWELI
Na Beda Msimbe
YALIKUWA majira ya saa mbili usikui, Ijumaa wakati nilipopita katika mtaa wa Majengo maarufu kama Kings Palice kati kati ya mji wa Mpanda.

Nilikuwa nimechoka lakini pia nilikuwa na hamu ya kujua usiku Mpanda ikoje na eneo ambalo niliambiwa linaweza kunipa taswira ya Mpanda usiku ni eneo la Majengo. Mtu aliyenielekeza hakuwa na muda wa kunipa hadhari, aliniona ni mtu wa makamo na ipo haja ya kukutanishwa na watu wa aina yangu katika maeneo ambayo ni wenye hulka fulani tu wanakuwa na uwezo wa kufika na kuvinjari.

Nilinyoosha miguu yangu kutoka Kenyatta, taratibu kama vile nina muda wote duniani, nikiangalia watu na miondoko yao hapa na pale na katika safari yangu kutoka mtaa wa Kenyatta nasikia harufu ya bangi hapa na pale, lakini ahh nilifikiri huenda si bangi ni majani yanachomwa moto.

Kwa siku ya leo Mpanda imeonekana usiku wake huwa mtulivu ukiachia muziki wa hapa na pale; maduka mengi ya bidhaa za kawaida hufungwa mapema zaidi, lakini maduka yenye bidhaa zinazofanana na maisha ya usiku hubaki wazi mpaka saa nne usiku na mengine kuendelea.

Katika muda huu nanyoosha miguu wamachinga wa mtaa wa Kenyatta walikuwa bado wanaendelea na shughuli zao japo wengine walikuwa wakifunga mafurushi lakini maduka ya pombe yalikuwa bado wazi na ya muziki pia. Katika mji ambao hadithi zake zina maingiliano makubwa na watu kutoka nje ya Tanzania na yenye uchumi unaonekana kukua kwa sasa, maisha haya ya usiku yasiyo na fujo yanaonekana kuwa ndio bora zaidi.

Dakika zilizidi kuyoyoma na kasi ya mwendo ilizidi kupungua kwa jinsi ninavyokaribia mtaa wa Majengo ambao wakazi wa hapa wameupatia jina la Uwanja wa Fisi. Nilitaka kukuficha ukweli, ukweli kwanini niliamua kufika Mtaa wa Majengo, maarufu kama Uwanja wa Fisi.

Nilipata tetesi kuwa upo ukahaba wa haja katika eneo hili na washiriki wake ni kutoka mikoa ya Singida, Mbeya, Tabora na kidogo Kigoma. Nikaambiwa tena kwamba wapo wanafunzi walioacha sekondari wakaenda katika kituo kile kikubwa kufanya ukahaba kwani unalipa.

Suala kwamba unalipa ni gumu kidogo lakini ukifika eneo unaweza kujua unalipa kwa kiasi gani. Naam nilifika eneo lile majira ya saa tatu na nusu kutokana na kutembea kuzembe kwangu, mambo yalikuwa ndio kwanza yanaanza kuchangamka lakini nilichotaka sikukikiona kirahisi vile.

Niliamua kuketi mahala kupata supu, kwa wale tuliozoea kuandika habari laini hizi, unapokosa dira, supu au pombe husaidia kuvuta muda kuona kuna kitu gani eneo lile. Katika supu, maneno yalikuwa zaidi kuhusu maadili makubwa, mambo ya machimbo. Watu wanazungumzia madini wanazungumzia utafutaji wa fedha wanazungumzia masoko na mawakala wanaowadhulumu.

Lakini katika mazungumzo haya, unaambulia kujua kwamba vijana wa eneo hili ambao ni mchanganyiko kutoka mikoa na nchi mbalimbali wana fedha za kukutandikia usoni kwa kukosa nidhamu wanayoitaka wao.

Wanachozungumza ni kuishi leo kama vile hakuna kesho, wakati unamaliza supu, wanaokunywa pombe sasa wanaanza kubadilika na hata wewe unaanza kuona kuna mabadiliko, mabinti ambao ulikuwa unawaona wana ustaarabu wanaanza kuvaa nguo zinazoashiria kuwapo kwa biashara.

“Hapa pana mambo,” nilisema nikitega njia ya maneno ili niweze kuambulia kitu. Kijana mwenye umri kati ya miaka 25 na 30 alinitazama kisha akatabasamu.”U mgeni wewe,” aliniuliza na mimi nikamwambia, ndiyo. Hapo ndipo alipoanza kutiririka kwani alisema ni eneo zuri hilo kwa biashara mbalimbali, wagumu wanaokaa migodini ndipo huja kuambulia asusa za maisha baada ya kuumia.

Pana pilikapilika sana hapa na kuwapo kwa madalali wa vyumba kuliniashiria kwamba kuna uwezekano mabinti hawa wanaofanya biashara wanamalizia mashauri hayo ya mapatano palepale, kumbe haikuwa hivyo.

Ukimuita binti pale, anataka muende naye ulikopanga, lakini si kutafuta pale ambapo pana madalali wa vyumba vya kupanga na madini, na bei yao waliwazaji hao kwa kukuangalia usoni ni nzuri lakini kimsingi Sh 5,000 inatosha kwa uliwazaji wa fasta.

Uwanja wa Fisi ni Uwanja wa Fisi kweli kama tabia za fisi zinavyojulikana kuna kila kitu kinachotakiwa kama ilivyokuwa katika uwanja wa Fisi wa Dar es Salaam, tatizo ni moja tu hakuna magodoro ya fasta eneo hilo, hakuna uwazi katika mipira japo baadhi ya gesti zina mipira. Nilipata nafasi ya kuongea na Agness (si jina lake la kweli) ambaye ni mwenyeji wa Mbeya.

Aliniambia kwamba amefika hapo kutafuta fedha kwa kuwa mji umeshaanza kuwa na watu ambao wanahitaji pia burudani. Alisema kuwepo kwa wageni wengi hasa wanaofanya mambo mbalimbali kuanzia usakaji wa madini, biashara za madini na vyakula wakiwa vijana wanafanya watu kama wao kuwa na sehemu ya kujipatia fedha.

Wanalipa vizuri watu hawa ambao alisema wengi wao ni vijana wa Kisukuma na hivyo na wao wanakuwa na uwezo wa kujisaidia na kusaidia wengine katika familia zao. Agness katika miaka yake ya 20 anapendeza kwa umbile lake lililojaa sihiri pamoja na kwamba bei yake yeye ni nafuu ya shilingi 5,000 tu bado hakuwa na uwezo wa kutengeneza fedha nyingi kama wenzake wengine, lakini amesema hakuna siku anayolala na njaa, wateja wapo.

Kwa watafuta huduma ya kuliwazwa, wanatumia fedha kwa kuwa kesho itapatikana fedha nyingine, machimbo yalikuwa poa sana, yalikuwa yanatema na biashara ya mahindi ni nzuri pia, fedha zipo Mpanda na mzunguko katika shughuli za aina hii upo kwa sana.

Ofisa maendeleo wa Mpanda, Grace nilipomuuliza kuhusu vijana kesho yake na matatizo wanayokabiliana nayo, alizungumzia mahitaji ya fedha kiurahisi kunachochea mambo mengi ambayo si mazuri ukiwemo ukahaba.

Anasema kwamba upo ubishi wa wazi na kutojituma miongoni mwa vijana, ingawa anajua biashara ya ukahaba inayofanyika Mpanda washiriki wengi si wakazi wa Mpanda, bali wageni waliokuja kutafuta fedha. Wapo wanaotafuta madini, wapo wanachimba madini na wapo waliokuja kufuata fedha za watafuta na wachimbaji madini.

Mpaka sasa hakuna mvutano wa wazi kati ya Polisi na makahaba hawa ambao kuanzia saa 12 jioni hutega mingo zao uwanja wa Fisi wakitarajia biashara hadi usiku wa manane. “Unaweza kuja hata saa nane hapa na kukuta loose, “ alisema Jovin (si jina lake) ambaye kazi yake ni dalali wa madini ya shaba.

Kwa wanafunzi wanaofanya ukahaba, labda ipo haja kwa taasisi za kiraia kutofumbia macho matatizo yanayoanza kuchipuka Mpanda kwani jinsi spidi ya madini inavyozidi kuongezeka ni dhahiri biashara ya ukahaba itashamiri na maambukizi ya magonjwa mbalimbali ya ngono yataanza kushika kasi na serikali mwishoni italazimika kutibia watu wake kwa fedha nyingi kutokana na ukweli kuwa mchezo wao ni mauti yetu.

KATAVI: Mkoa ulioondoa ubabaishaji katika siasa
Na Beda Msimbe

PASI shaka ukiacha Arusha, mkoa wa Katavi unaotokana sehemu kubwa na iliyokuwa wilaya ya Mpanda, Chadema ina nguvu ya kutosha na miaka mwili iliyopita ilikuwa ni kama watia mafuta katika moto, kulikuwa na ukakasi mkubwa katika siasa.

Ukakasi huo ulifanya sehemu kubwa ya shughuli za maendeleo ama kusuasua au kudumaa kutokana na mvutano wenye lengo la kuonesha nani mbabe katika siasa za kuendesha maeneo.

Lefi Matongo ambaye ni kiongozi wa chama cha CHADEMA na diwani wa kata ya Kashaulili kati kati ya mji wa Mpanda katika mazungumzo anasema hivi sasa ni shwari, Katavi kutokana na ukweli kuwa hivi sasa siasa za ubabaishaji zinaelekea mwisho.

Nilipotaka kujua zaidi nini kinatokea alijibu kwa utaratibu sana:” Hii ni kutokana na wananchi wengi kuwa na uelewa kuhusu mambo mbalimbali.” Ni kweli huenda siasa zimepanuka sana na kuwafanya watu wawe na taratibu za kuvumiliana ingawa ni dhahiri bado yapo maeneo ambayo siasa zinatakiw akubadilishwa ili kukidhi haja ya maendeleo katika mkoa mpya.

Eneo la Karema kandoni mwa Ziwa Tanganyika siasa zinababatiza sana maendeleo kwani hata mtendaji wake alisema hadhani kama watu wanafikiria vyema wanaposhindw akutafakari mahitaji yao, nguvu zao na haja ya kutoitegea serikali katika ustawi wa jamii.

“Unauliza siasa ndugu mwandishi, hapa siasa ina shida vyama vinazuia maendeleo, hata Diwani wa hapa ambaye ni wa CCM naye anaendesha siasa zisizoeleweka anawataka wananchi kutochangia maendeleo” alisema mtendaji huyo,katika mazungumzo huku tukiwa katika eneo linapojengwa bandari mpya Karema.

Pamoja na karema kuonekana kuwa na tatizo lakini kw aujumla vingunge wa siasa wa Katavi yaani Chadema na CCM wanakubaliana kwamba hali kwa sasa imebadilika sana na watu wa Katavi wanashirikiana katika kukabili changamoto zao katika sekta ya maji,kilimo na elimu.

Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Katavi, Abdalah Mselem yeye anashukuru kwa mshikamano uliopo baina ya viongozi wa siasa mkoani kwake ambao unaonesha kukomaa kisiasa. Anasema Katavi kwa sasa wanaupinzani usio wa vitisho wala chuki binafsi na hivyo wanachama wa vyama tofauti vya kisiasa wote wanashirikiana katika misiba na harusi.

Katika mahojiano na Mkuu wa Mkoa wa Katavi Dk Rajabu Rutengwe kuhusiana na hali ilivyokuwa miaka miwili iliyopita na sasa alikiri kuwa mkoa wake umepiga hatua kubwa katika mahusiano. “Tumefanikiwa kukuza mahusiano kati ya serikali, Chama tawala na wapinzani na hivyo kuongeza kasi ya kusaka maendeleo miongoni mwa wananchi wetu” alisema Dk Rutengwe kwa kujiamini.

Dk Rutengwe ambaye kabla ya kuwa mkuu wa mkoa huo mpya alikuwa mkuu wa wilaya ya Mpanda alisema hivi karibuni katika mahojiano na gazeti hili kuhusu hali ya kisiasa ilivyo kwa sasa mkoani humo kuwa kwa sasa hakuna hali tete.

Alisema, ingawa miaka miwili iliyopita hata kabla ya kuanza kwa mkoa mpya hali ya msuguano ilikuwa tete,kwa sasa hali hiyo haipo na kwamba wananchi wanaanza kuelewa umuhimu wa kusukuma mbele kazi za ujenzi wa taifa huku upinzani ukibaki katika hoja zaidi kuliko hitilafu.

Kipindi cha nyuma msuguano mkubwa ulikuwepo kati ya mashabiki wa Chadema na mamlaka mbalimbali za serikali na chama tawala hasa katika masuala ya maendeleo. Mbunge wa Mpanda Mjini na Makamu Mwenyekiti wa Chadema, Said Amour Arfi, anadaikuwa kuwa chachu kubwa ya mabadiliko kutokana na jinsi anavyokabiliana na wanachama na mashabiki wenye jazba wa chama chake katika mkoa huo.

Mwandishi mmoja wa habari ambaye nilipata nafasi ya kuzungumza naye katika kupanuana kuhusiana na suala la siasa katika mkoa mpya alisema kwamba kama si Arfi kutia mikono na miguu yake kila mara na kila mahari huenda yanayotifuka huko Arusha yangelitokea na hapa.

Ukizingatia ukweli kuwa Katavi kuna kambi ya wakimbiziambao wengi wao hawakusalimisha silaha walipoingia, kuwepo kwa mitikisiko ya kisiasa isiyozingatia hali halisi ingelikuwa balaa kubwa kwa mkoa huo mpya na taifa pia.

Kambi ya Katumba iliyopo Katavi imebeba sura nyingi na inaweza kutumiwa kisiasa kama watu wasipokuwa waangalifu na kutulia kwa hali ya kisiasa kunatokana na vinara wa usalama (Vyama husika vya siasa) kutambua hilo na kuamua kushirikiana kuhakikisha kwamba wanakomesha ujambazi na kutotumika kuharibu amani na maendeleo ya mkoa.

Katika mazungumzo Dk Rutengwe alisema Kwamba serikali ya mkoa ilifanyakazi kubwa ya kuondoa na kudhibiti mawazo hasi ya kimaendeleo ambayo yalikuwa yanakwamisha juhudi za kumkomboa Mwanakatavi.

“Maendeleo yataletwa na wanakatavi wenyewe;kubuni,kupanga, kutekeleza mipango yenyewe inawezekana tu kwa kuwa na utashi usiozingatia itikadi bali hoja muhimu ya maendeleo” alisema Mkuu wa mkoa na kuongeza kuwa wananchi wa Katavi kwa sasa wanatambua kwamba kuna umuhimu wa kuhimizana maendeleo na si siasa za majitaka.

Mkuu wa mkoa alisisitiza kwamba mkoa wake wenye dira ya maendeleo ya miaka 20, dira ambayo inawaelekeza wanakatavi namna gani waende na kuweka maeneo yao katika hali tayari kuchangia uchumi binafsi wilaya,mkoa hadi taifani haiwezi kufanikiwa kama siasa zitakuwa hovyo, ndio maana muda mwingi ametumia kutengeneza amani ili dira hiyo itekelezwe na wananchi wa Katavi wafaidi mali asili zao.

Kwa mujibu wa mkuu wa mkoa mpango huo umegawanyika kati ya muda mrefu na muda mfupi, mpango ya muda mrefu ikilenga pamoja na mambo mengine kuiwezesha Mpanda kupata hadhi ya manispaa, siasa za wastani zinazoonyeshwa sasa zisizokuwa na jaziba zitaifaidisha.

Hata hivyo mkuu huyo wa mkoa alikiri kuwapo kwa changamoto kadhaa ambazo zinaweza kabisa kusaidia watu kupingana bila jazba bali maendeleo. Kauli yake hiyo inafanana kabisa na matamshi ya Thomas Ngozi mzee maarufu katika mkoa wa Katavi .

Mzee huyo anasema inaonesha hivi sasa siasa zinabaki ni za vijana kwani kumekuwa na wigo mpana sana wa kutoa fursa kwa vijana hivyo ni mategemeo yake kwamba watatumia busara za wazee kutengeneza amani kwa ajili ya maendeleo ya mkoa wao.

Wakati wa mazungumzo alikuwa muda wote akiwataka wakuu wa vyama kusisitiza amani na kuipa kipaumbele katika siasa zao badala ya kuhangaika kuchovya maneno kwa lengo la kushika dola pekee na kuacha mambo yanaharibika.

Kwa mkoa wenye kuamka na kuwa na shughuli nyingi za madini na tarafa sita za utawala zilizotawanyika katika mbuga kubwa na ndogo ni dhahiri utulivu wa kisiasa unaweza kabisa kutumika kutengeneza maendeleo na kuzuia kuporwa kwa mali ya mkoa huo.

Tarafa kama za Karema, Mwese, Kabungu, Inyonga, Nsimbo na Mpimbwe zinaotengeneza kata 33 zimetawanyika sana katyika Hifadhi ya taifa ya Katavi huku nyingine zikiwa katika hifadhi ya Inyonga inayozalisha asali.

Ni dhahiri utekelezaji wa dira ya maendeleo ya miaka 20 katika mkoa ambao ndio kwanza unaanza safari ya maendelkeo huku ikiwa na raslimali nyingi ambazo unatakiwa kufanywa kwa mashirikiano makubwa kati ya waqzawa, wageni na wanasiasa, serikali yenyewe ni kusimamia mipango hiyo.

Mashirikiano ya makundi ya kikabila kama Wabende, Wakonongo, Wafipa, Warungwa na Wanyaturu ambao wanaishi Inyonga, Karema na Mishamo kwa upande mmoja na Wapimbwe, Wanyarwanda, Wachaga, Wasukuma na Wamasai wanaoishi Mpimbwe, Mwese, Nsimbo na Ikola kwa upande mwingine utakuwa ni faraja kubwa.

Makundi haya ya makabila ambayo mengi ni ya wafugaji na wawindaji utulivu wa kisiasa utawezesha pia kudhibiti matatizo yanayotokana na ukimbizi . Katavi ina makambi mawili ya wakimbizi ya Mishamo na Katumba yanayohifadhi watu wa kabila la Wahutu kutoka Rwanda na Burundi kuanzia miaka 1972 japokuwa wengi wamepewa ukazi,makubaliano yao ya ukazi bado kutekelezwa.

Siasa za Katavi pia zinasaidiwa na kuwapo kwa machifu wa kikabila ambao wanatumika kurekebisha mambo katika jamii. Machifu hawa pia wamemtambua mkuu wa mkoa kama Chifu wao mkuu kiasi ya kwamba maagizo ya serikali yamekuwa yakiwafikia na kuyasimamia kwa maslahi ya umma.
SAA 37 ZA DAR HADI MPANDA
.Mama moyo wangu! yaani mashaka na hofu  barabarani,msituni
.Dereva macho pima, abiria mapenzi, kinywaji,kuchimba dawa
.Kondakta gari halijai si ndoo ya maji,sogea kule,ukiwa mzee balaa
 Habari Na Beda Msimbe
NIMETUMIA takribani saa 37 kutoka Dar es salaam na kufika katika makao makuu ya mkoa wa Katavi, mji unaonekana kubadilika kwa kasi wa Mpanda.Na ninachoandika hapa si hadithi ya kubuni ni ukweli nikichukua muda hadi muda.
Majira ni saa kumi na nusu alfajiri,naamshwa na watoto, nisije nikachelewa kwani basi linaondoka saa moja kasoro robo na kwa utata wa usafiri wa huku kwetu nikaapo ni lazima ujihimu kidogo.Saa kumi na moja na dakika 15 naondoka nyumbani na dakika 25 baadaye nafika stendi ya kunipeleka Kimara, hakuna basi , muda unaenda naamua kuchukua pikipiki.
 Saa kumi na mbili na nusu ninafika Kimara, nasubiri basi litakalonichukua hadi Mpanda kwa kupitia Mbeya na Sumbawanga, sikujua kwamba nitalazimika kulala Mbeya, wenyewe waliniambia kwamba niwape 67,000 na nitafikishwa Mpanda hawakunipa hadhari kwamba ni lazima nijitegemee kulala Mbeya na tena nikifika Sumbawanga ni lazima niingie katika gari nyingine na hivyo kuhamisha mizigo yangu.
 Moja kasoro nikawapigia simu kwamba abiria wenu wa Kimara nawasubiri,wakaniuliza gari la saa ngapi,nikawaambia la moja kasoro wakasema linakuja wakanitajia gari namba 616 kwamba ndilo litakalonichukua kuelekea Mpanda, mkoa mpya wa Katavi.
 Wakati nashangaa kunataka kutokea nini pale kituoni daladala akabanana na basi ninalosafiria,akalambwa kioo nikasema ohoo ishakuwa nuksi tena, manake hapa hamjatoka Dar, dereva kaonesha kutojua upana wa gari lake.Nikalifuata pale nikaingia, wakamalizana tukaanza safari kuelekea Mpanda.

Mbezi tukachukua abiria mbele kidogo tukaanza mwendo. Basi lilitakiwa kuwa lakshari, lakini haa, ndani utadhani halikaguliwi na Sumatra manake viti hovyo, mikanda haipo na stuff carrier ilionekana kama inataka kuachia japo ilitengenezwa kama yale ya kwenye ndege.
 Mhh sikuwa pekee yangu aliyeshangaa, mtu aliyependa Mbezi naye alishangaa, wale waliokuwapo wakasema what kind of a car, ilikuwa kiinglish lakini matamshi yake yalifanana na watu wanaotoka Zambia, Wanyanja wakijiuliza ni aina gani ya gari wamo,kwani wanatazama mle ndani silo walilooneshwa jana yake wakati wakikata tiketi linapiga madebe kwelikweli kwa ndani.
 "Halafu konda hii bei ni ya lakshari kinywaji kipo? manake basi lenyewe halielewekieleweki" alijibiwa kiinywaji kipo lakini  he Dar hadi Mbeya tulipewa kwa lazima Cocacola ya kwenye plastiki hawakuwa na kinywaji kingine na wala maji hawakutoa.Walitupa kinywaji hiki kabla ya kuingia Doma, mara tu baada ya kumaliza kuchimba dawa.
Mbali baada ya kuanza kupata mwendo tukaingia foleni ya Kibaha na mbele ya Kibaha akapanda mama analalamika kwelikweli kaachwa na basi la kampuni hiyo,kumbe asubuhi kampenuni ile iliamua kukodisha basi bila taarifa kwa watu wakajiendea tu,.
 Njiani jamaa anaovateki magari matatu manne na unajua barabara ya Dar-Chalinze ilivyo ikiwa na mibinuko ya ajabu, jamaa anazipangua anaziweka, hapo roho inaanza kuwa mkononi, unashangaa umpigie Mpinga au nani barabarani na namba walizosema wanaweka kwenye mabasi pale haipo, unakula uchungu , mama moyo wangu! breki vuu, ghafla mnaingia kushoto. Mashaka barabara ya lami.
 Haya  bora salama, Mungu anasaidia mnaacha miti ikirejea nyuma na nyie mkisonga mbele mnaingia Morogoro, stendi ya Msamvu unapumua,mnapakia abiria wengine, wanatoa chati kwa Sumatra na Polisi wanaikagua wanaruhusu mnaingia barabarani tena mnaanza kuitafuta Mikumi, Mbele kidogo kabla ya kufika Doma  Kondakta anaelezea suala la kuchimba dawa. Wazungu kama tisa hivi waliokuwa mle ndani hawakuelewa nini kinatokea.
 " kuchimba dawa, anashangaa .. "kuchimba ni to dig, dawa medicine maana yake nini hasa" akajiuliza mtu aliyeonekan anajua kiswahili zaidi na wenzake walitaka maelezo.Watu hawakuzungumza Kiinglish lakini walipoona, watu wanateremka waliteremka na wakabaini kwamba ni suala la kujisaidia.
 Unakumbuka maneno  ya kuwa na vyoo kwa ajili ya abiria njiani , choo kile kinauwezo wa watu watatno, abiria sitini, wengine na wazungu kadhaa waliingia msituni huku  karibu na barabara kunagulio la nyama.
 Mnamaliza kuchimba dawa mnaingia , mnapita mbuga ya mikumi na spidi 110 wakati wenyewe wameweka matuta na kusema spidi inayofaa ni nusu yake, unashangaa mkikutana na tembo, ama tembo ama nyie.

Njiani sasa simulizi zinaanza zimeanzia katika suala la kuchimba dawa. Masimulizi yanahama kushutumu serikali na matamko yake,wakaingia hapo kuzungumzia urais na nia za akina fulani wakiwataja kwa majina kwamba wanawania Urais huku wakiwa wagonjwa na wala hawawezi kabisa kuongoza taifa.
 Siasa za kuanzia Morogoro hadi Comfort zilikuwa za wastani, wakichamba elimu na kusifia namna watoto wanaojifunza Uganda walivyokuwa na akili kuliko Tanzania kwa kuwa wanajua kupepeta Kiingereza.
 "ahh kwa wale wa Uganda labda kiingereza lakini uchambuzi na uelewa bure kabisa" niligeuka kutazama wanaozungumza nikagundua ni vijana. Hawa walibishana kwelikweli manake walisema kwamba mfumo wa elimu tanzania bado ni bomba  mwingine akisema kwamba si kweli elimu ya tanzania imeoza watu wanajiumajiuma katika kujieleza.
 Comfort, pale Kitonga tuliingia mapema,pamoja na ukweli kuwa enoe limechakaa, hata akili za watu zimechakaa sana kwani wanauza bidhaa kama wapo Mogadishu, aina moja bei ghali urafiki haupo  bure kabisa.
 Mnamaliza  mnaondoka, mtu na mkewe (vijana) gari limepiga mijihoni hawakusikia wala kuona na  asali zikiwamiminika (si bure wameona juzi hawa) tuko juu kelele mtindo mzima, bahati yao tulikuwa bado kuingia barabara kuu na mzee moja akashtuka kiti kimoja hakina abiria.
 "Mmeacha mtu na mkewe" anasema  huku mtu njiani mbele anapunga bkw anguvu kuashiria watu wanaokimbilia gari.Walipanda hawana hata sura ya hasira wakaendelea na asali zao.
 Kitonga ilipandishwa kama tambarare, siasa zikaelekea kwenye shimo kubwa zaidi nani anafaa kuwa rais, wote wakawa wanajadiloiana wagombea wa CCM badala ya kuangalia na vyama vingine unasema kaazi kwelikweli.Ukimtazama dereva, haongei na mtu anabadilisha gia,anakanyaga mafuta huku mguu upo kwenye brekiu kama anaibia vile, staili ngumu zaidi. Kwa mwendo ule lazima awe macho pima.
 Saa tatu mnaingia Mbeya, unadhani mnaendelea:"wale abiria wa Mpanda na Sumbawanga tukiingia mjini mfike ofisini kwa maelezo, mshuke na mizigo yenu"
 Kweli tulifika maelezo ni kuwa uripoti saa kumi na moja na nusu na basi linaondoka saa 12 kamili kuelekea Mpanda nba wale wa Sumbawanga wakaambiwa saa mbili asubuhi. Wapi pa kulala, mzee sio ndege uko tranziti, wewe tafuta gesti zipo nyingi la maana kesho uawahi.
 Naam linakushuka,usiku wewe mgeni, unampa mtu buku anakutoa kidogo stendi anakufikisha gesti inaitwa sinahela. Unalala, umechoka hata hujui itakuwaje saa kumi na moja hiyo unaomba msaada wa kuamshwa na mlinzi. Unagusa maji ya baridi, unauliza maji vipi unaletewa maji ya moto unaoga na fasta unalala.

Wala uhitaji kuamshwa kwani usingizi wenyewe unao,?Anafika kukugongea anaukuta wewe unatoka kuoga angalau uchangamke. Unasubiri kupambazuke unauliza je salama anakuambia salama. unaondoka na kufika stendi.
 Unauliza ofisini basi la kwenda Mpanda wanakuambia mngoje mhusika. Mhusika haji unatoka nje unaenda katika magari unauliza la Mpanda wanakuonesha unasema duhh hii kali unaingia kukaa katika kiti cha pembeni aliyekaa kala kiti kimoja na nusu halafu unajiangalia mwenyewe.
pembeni mwako wapo watu na asubuhi ile wanazungumzia siasa, masuala ya sensa na jinsi wengine walivyogomea sensa.
 Siasa za kuanzia Mbeya kuelekea Mpanda zilikuwa ni ukali wa Chadema,na kutokuwa wavumilivu. he mwenzio kama jamaa yangu na khanga yake ya CCM kafua kaianika wanakuja watu wenye nyumba wanaanza nani kaweka balaa hili atowe mara moja, khanga ile si ilikuwa na maji wakamlaimisha aiondoe pale.
 "Jamani chadema sijui vipi yaani washari shari".
 Tukaondoka kondakta akisema wazi hataki mtu wa kusimamisha huku dereva akilalamikia upangaji mbaya wa mizigonutamletea taabu kwenye mizani. Tuliondoka njiani kote hakuna kupandisha wala kuongeza tukapita mizani, tukaingia Tunduma tulipoachana na Polisi wa Tunduma na kutokomea zaidi katika barabara ya vumbi inayojengwa, basi lilikuwa halijai labda ndoo ya maji.
 Akaingia mtu mzima akaona haina maana akaweka begi lake, akalikalia konda akasema we wala bibi hakujibu, mdada mmoja akasema mhh wazee hawa wana lao, jamaa anasema wala hamjibu anayetaka kupita aende nyuma yake na apite tu, anagemesha bega lake pembeni umruke. Inayojaa ndoo ya maji si basi.
 Njiani wanapanda wawili, mvulana na msichana inaonekana wanajuana. wanakimwaga cha nyumbani lakini mvulana akamuona demu mmoja rangu ya chungwa amesimama, akamwambia binti aliyeingia naye aanzishwe swaga za mapenzi, jamaa alisahau kwamba kibantu tunasikilizana kwa asilimia 50 nikafuatilia maagizo.
 Mapenzi yalinoga sana katika gari hili la Mbeya kwenda Mpanda. Jamaa alikuwa tayari kumshusha Laela binti wa watu na kumpandisha gari kesho yake, mtoto akamsikiliza akamtolea nje.Akasema anajeuri ya fedha alikuwa anafika laela kununua spea ya pikipiki yake, kisha simu hiyo inayothibitisha kwamba ni dereva wa pikipiki jamaa anatafuta usafiri akamwambia yupon garini anaenda laela kutwaa spea ya waya wa eksereta umekatika.
 Anamaliza anaendelea kumpelekea rapu za mapenzi msichana yule hadi anafika laela akitaka kumpa fedha za kushika:Nikasema watu wanahatari humjui mtu katoka wapi unataka kushuka naye.

Masikio yangu yalikuwa na utamu mkubwa, huku mapenzi, huku uongozi ujao na katiba huku mama mmoja akisema kwamba haoni sababu ya kupiga kura,wengine wakisema ni wajibu wake kuchagua viongozi.. wewe wanakusaidia nini au tuseme wameshakusaidia nini.
 Masikio yangu yalinogeshwa na siasa,mapenzi yanaendelea na kisha inakuja suala la barabara. Vumbi linatimka watu wamefunga vioo  kondakta akagundua wageni wengi ndani ya basi. jamani msifunge vioo tutakufa  wacheni vumbi liingie na kutoka. Basi limejaa ndindindi. lahela sick love boy akashuka na mbele kidogo tukanasa katika maji madogo kwenye barabara inayotengenezwa.
 He tunashtukia tunaelekea katika majumba ya watu basi limeacha njia, vile vimaji kidogo katika barabara viliharibu kabisa eneo tunalopita. maji yale yalimwagwa katika barabara inayojengwa. Mhh ilituchukua dakika 15 kutoka hapo, watu wengine waliamua nkutumia muda huo kuchimba dawa.
 "hawa wajanja wanataka kumaliza barabara hii muda mfupi nkabla ya uchaguzi kujipa maileji" anasema mtu mmoja.Ahh tunajenga na madafu yetu tunachelewa kodi hatulipi.. hapana bwana fedha hizi mbona ni za MCC. " Nakuambia kumbe watu wanajua na uwezo wa kubishana upo, wanasema kuhusu uchelewefu halafu wanauliza rais kwanini alimuondoa Magufuli.
 Baada ya kukamata mwendo sasa ukafika muda rasmi wa kuchimba dawa, watu waliposhushwa kulikuwa na mti wa matunda pori, wenyeji wanajua wakaanza usijisaidie hapo( kwa lile neno halisi) kuna matunda , watu wakenda mbali kujisaidia wakirejea wanachukua matunda hata dereva ilituchukua muda kuondoka hapo.
 Kutoka nhapo ikawa pandisha shusha,ingia kushoto ingia kulia mpaka tukafika Sumbawanga saa 9 na nusu.nimechakaa kwa vumbi na kutokuwa na mahali pa kuegemea. nabanwa na mwanamama aliyejaliwa na katikati kuna mtu wa kufa mtu wamesimama.mambo hayo nikatulia watu wakawa wanashuka. Mara mzee kama unaendelea Mpanda ni basi hilo la pili hili hapa ndio mwisho wa safari.
 Maskini mie nabadilisha basi mara ya tatu kw atiketi moja ya Dar-Mpanda. Nikachukua  vitu vyangu nikaingia basi la pili, hapana mzee kwanza ofisini ukabadilishe tiketi.Vitu vyangu? Hapa Sumbawanga atakayekuibia lazima awe taahira.,
 Unaweka begi kubwa unaondoka na beki lako dogo lenye vifaa vyako vya kazi.
 Unabadilisha tiketi. Unaingia msalani kumeandikwa bei 200 unatoa hela unaambiwa bei 300 zi ile iliyoandikwa.
 Basi linaondoka saa  kumi hapa Polisi wanafanya kazi yao wanasema zipo namba kama dereva anajaza au kukimbia tupigieni safarini salama. kweli basi lile lilikuwa na namba za RPC wa Rukwa, Mbeya, katavi na Dodoma.  Mnaanza safari,mazungumzo hapa yanabadilika, watu wote wamechoka wanatazama saa, simu zinaanza kuingia.

Kila anayejibu analalamika kuchelewa kwa gari, kumbe tulitakiwa kuwa Sumbawanga saa saba ili saa moja tuwe Mpanda.
 Jirani yangu akanisimulia jinsi ilivyo hatari kusafiri usiku na kwamba basi lile lilishawahi kufanyiwa kitu mbaya na dereva yule yule. Watu walikusanywa simu na fedha huku mkusanyaji akiwa ni dereva wa Fuso lililotekwa kabla yake.
 Paniki zinaanza kuingia, huwa natembea na chuo kidogo cha sala, pamoja na kumuomba raphael, malaika mkuu kuwa nami safarini pamoja na abiria wengine na kumchunga dereva asifanye maamuzi ya kipuuzi nilianza safari ya mateso ya Kristo, kuomba ulinzi kamili kwangu , basi na abiria wengine kwa maana kulikuwa na wanawake wengi katika basi na watoto na kila mmoja kwa namna fulani alionekana kugwaya.
 Dereva alichapa mwendo na wakati kiza kinaingia tulikuwa njia panda ya kwenda bandari ya Debwe, dakika 15 za ukweli zamkuchimba dawa, hakuna hata choo cha kulipia watu wakajitoma katika vichaka vichafu unachagua tu pa kuweka uchafu wako pia.
 Dakika 15 ziliisha na kisha tukaanza mwendo tukaingia katika Mbuga kila mtu alikuwa kimya mbele kidogo kwenye kiteremko kibaya gari likasimama, akashuka Kondakta, mara dereva akasema Hassa mbele yako simba, watu wote wakataharuki, mama mmoja akafungua simu akaanza kusoma duwaa,kiza kilikuwa kimetenda.
 Yule mtu akaingia tukaanza taratibu kushuka,mama mmoja jirani yangu akasema pale si pazuri hata kidogo wakiweka mtego hatuwezi kupona, lakini jambazi anayekaa msitu wa simba naye lazima awe kanuia kufa. Lakini ni katika hifadhi watu wanatekwa. Paniki, nikasema damu azizi ya Kristo iliyomwagika msalabani tuondolee kiwewe. hata ile ya Getsmane sikuikumbuka. Kila mmtu alionekana kivyake sana.
 Saa mbili usiku bado tupo katikati ya msitu, unaowaka moto na baadaye tukaupita tukakutana na magari kadhaa na saa tatu kasoro tukaona umeme, dalili ya kumalizika kwa msitu,lakini kumbe watekaji nayara ndio maeneo yao, kijiji cha kwanza tu kutoka mbugani.
 "Naomba nishuke ..."sikusikia alisema kama kwa kilugha lakini aliyeshuka usiku ule eneo lile lisilokuwa na umeme alikuwa na watoto sita akiwemo mchanga mgongoni, watu wakasema jamani usiku na watoto,ulikuwa usiku lakini kile kilikuwa kijiji, mbele watu walikuwa wakitembea.
 Tulipiga mwendo, mbele zaidi kiboko akawa ametulia katikati ya barabara.Jamaa akafunga breki akazima taa akawasha. akazima tena. Alipowasha kiboko yule akajiondoa pale barabarani tukapita.
 Saa nne tunaingia Mpanda hoi bin taaban, kasheshe za kutafuta mahali pa kulala.Muungwana mmoja alifika akanipokea akanifikisha nyumba ya wageni,tukala saa tano na sita kamili nilijitupa kitandani sikujua kinaendelea nini.

LICHA YA KUVUNJWA UWANJA SOKA LINAENDELEA
Na Beda Msimbe, Mpanda

PAMOJA na kuvunjwa kwa uwanja pekee wa michezo wa CCM mjini hapa,Chama Cha Soka kimesema kwamba kinakamilisha maandalizi ya kuanza kwa ligi daraja la nne.

Hayo yalisemwa na  Mwenyekiti wa chama cha soka cha hapa, Seif Bakari.

Uwanja huo ambao enzi za Katavi Rangers ulikuwa uwanja wa pili wa nje ukiachia Kaitaba kwa kuingiza  mapato ulibomolewa wiki ya jana na watu wa Tanroads, katika kuwaondoa wavamizi wa hifadhi ya barabara.

Bakari alisema kwamba mpaka sasa timu 7 kati ya zaidi ya 12 zimelipia ada ya ushiriki. Hakutaja timu hizo.

Alisema pamoja na kuvunjwa kwa ukuta wa uwanja huo, wataendelea kuutumia kwa kuwa hakuna uwanja mwingine.Ukuta wa uwanja huo unaotazamana na barabara ndio umevunjwa.

Alisema hata hivyo ligi hiyo imechelewa kuanza kwa kuwa chama chake kimekuwa kikiratibu  mashindano ya shule za sekondari yaliyodhaminiwa na mbunge wa Mpanda Mjini,  Said Amour Arfi ambayo sasa yapo katika hatua za fainali.

Mashindano hayo yaliyoshirikisha sekondari zote yalilenga kuibua vipaji vya watoto na kuviendeleza.

Sekondari zilizoingia katika fainali za michuano hiyo ni Mwangaza na  Misunkumilo.

SEIF BAKARI: Beki wa zamani anayemhusudu Hussein Ngurungu 'bwana mipango'

Na Beda Msimbe,Katavi

" Utamu wa mpira ni kufunguka bwana, wakati mwingine suala hili la kupaki basi linaudhi sana, hupati utamu wa mpira.. mpira ufunguliwe ndio mpira unapendeza" anasema beki wa zamani wa  timu za Urambo, Coastal Sport na Ujenzi , Seif Bakari.

Beki huyo ambaye  bado mwili wake upo katika fomu na ni kiongozi wa chama cha Soka Mpanda anasema raha ya soka ni namna inavyotandazwa na namna  mshindi anavyopatikana kutokana na ufundi wa kutandaza gozi.

Anasema ipo haja ya timu kuonesha uwezo wake, zicheze kabumbu na mwenye uwezo atwae ushindi .

Bakari ambaye anasema kwamba soka limemsaidia sana anasema ipo haja ya kuwapo kw ampango wa kuibua vipaji kwa kuwa na shule maalumu na kusema TFF inahusika katika hili wanawjaibu wa kushiriki katika kuwa na akademi za soka nchini.

Bakari ambaye alifanikiwa kumdhibiti 'bwana mipango' Hussein Ngurungu ambaye alikuwa katika timu ya taifa kwa miaka kumi  anasema analiheshimu soka kwa kuwa ndilo lililompatia kazi.Bakari anasema hawezi kudharau soka japokuwa watoto wake hakuna hata mmoja aliyemfuata.

Bakari  ana watoto sita lakini hakuna hata mmoja aliyetaka soka wala netiboli.

Bakari ambaye enzi zake alikuwa anacheza nne,tatu na mbili amesema kwamba aliacha gemu kwenye miaka ya 1980 na kuanza kufundisha kutokana na maumivu ya enka wakati akiwa anacheza Ujenzi Rukwa.

Pamoja na kuacha soka katika uwanja aligeuka kuwa mwalimu wa soka na kuanza kufunza Ujenzi Rukwa, Katavi Rangers na Super Star maarufu kama Kakukuku. baadaye alianza kufundisha timu za watoto kwa kushiriki kikamilifu kunoa Mwangaza sekondari kwa miaka minne kuanzia miaka ya 1986 hadi 1989.Kocha huyu anasema kwamba anajivunia watu kama akina Muddy Sumri, Revocatus Kalumbe na Tabuye Mrisho ambao walikuwa katika timu ya Katavi Rangers.

Ingawa kwa sasa yeye ni mwenyekiti wa chama cha soka Katavi, Bakari alisema kwamba  kwa sasa mchezo wa soka kwa sasa ni gharama kubwa mkoani katavi hasa katika uendeshaji na uwezeshaji. Kwa mkoa wa katavi ambako wadhamini ni wachache, mwalimu unajikuta unafanyakazi zote za ukapteni, umeneja na kufanyia kazi kero mbalimbali ambazo hazimo katika utaratibu.

Anaamini kwamba kama wakiwezeshwa wanaweza kwenda mbali zaidi kwani soka ni mafunzo,soka ni mazoezi na soka ni kujituma.

Akiwa amezaliwa 1954 maeneo ya Mwanga mjini, Kigoma na kupitia shule za Mwanga Extended na Kigoma sekondari anakumbuka watu aliotia nao ndinga kama akina Daudi salum, Abdallah Mwinyi Mkuu na Kitulo ambaye kwa maneno yake mwenyewe alimwaminia sana namba tisa hiyo.

Bakari ambaye kwa sasa ni fundi sanifu mkuu  umeme na elektroniki mkoani katavi anasema anakumbuka jinsi alivyomkaba Hussein  Ngurungu wakiwa Tabora pamoja na kwamba bwana mipango huyo alikuwa anakimbiza kikwelikweli. Anasema alimkaba  bwana mipango na hakuweza kutikisa nyavu za timu yake hiyo ya Tabora.

"Lazima ujisifu kama unaweza kumdhibiti bwana mipango, na siku ile nilimwambia hupiti na 

hakupita'alisema Bakari.

Alisema nyakati hizo zilizopita Mukebezi na Chuma pia walimfurahisha sana wakiwa  uwanjani,pilikapilika zao zilikuwa zinatisha kama Hussein Ngurungu alivyokuwa anatisha.

Analionaje soka la sasa.
Zinahitajika juhudi kubwa kufua vipaji kwa kuanzisha shule za vipaji kwani vinasaidia sana kutambua na kutunza vipaji, hata zamani shule kama Kazima iliwika kwa kutoa wanaojua soka kiufundi sana, 

Mwalimu wa hapa aliwachukua hata watoto waliokuwa hawakufdanya vyema na kuwaendeleza,huu ulikuwa upenzi wake.

Niseme kwamba upenzi ndio ulikuwa uliifanya Kazima wakati huo kuwa na sifa ya vipaji vya wachezaji  ilikuwa inatunza vijana wanaojua nini wanakitaka katika michezo na Mwalimu wa hapa alikuwa anazingatia hilo.

Anasema pia vilabu kama Yanga na Simba havina budi kuimarisha timu za watoto kama nyakati za Victor Stanslaus aliyeweza kuwatoa watu kama akina Juma Pondamali na Matokeo."Bila kuwa na timu za watoto na kuwafunza hakuna maendeleo ya soka, tutabaki tunanunua wachezaji magarasa ambao 

thamani yake ya fedha ni duni " alisema Kauli yake hiyo aliisema kwa mfano na kuuliza kama kweli wachezaji wa kigeni waliopo Yanga na Simba sasa wanawazidi watoto walioiva wa hapa nyumbani kwa thamani ya fedha wanapokuwa viwanjani."Kutegemea wachezaji wa kununua wakati wote ni tatizo", alisema Bakari.

Pamoja na timu za watoto mikoa inastahili kuwa na shule za vipaji maarufu kama akademi ambapo shirikisho la soka nchini (TFF) nao wanatakiwa  kutia mguu kusaidia." Hili TFF hawawezi kulikwepa la kutengeneza wachezaji wajao" alisema Bakari na kuongeza wanaweza kwa kushirikiana na wadau wengine.

Amesema katika kawaida ni lazima kuandaa watoto katika kutengeneza soka lijalo vinginevyo 
hakutakuwa na soka tutabaki tukilalamika.

"Tusipowezekeza tutaendelea kuchukua wachezaji wa kigeni wasiosaidia timu kuwa na uwezo wa kushinda na kucheza kwa pamoja" alisema Bakari.

Dhana ya uchawi sokani

Mimi naamini kwenye mafunzo, sio katika saikolojia ya wachawi kwani  kama ni hivyo basi watu wa Katavi na Rukwa kwa jinsi wanavyotusifia tungelikuwa tuko mbali sana katika soka lakini sivyo.

Alisema hayo wakati  mwandishi wa habari hizi alipotaka kupata kauli ya uzoefu wakati akicheza na timu kubwa kuhusu nguvu za kiza katika kuamua ushindi graundini.Alisema yeye haamini katika hilo ila anajua wapo watu linawapendeza likiwa hivyo.

Alisema mara nyingi si tatizo la kocha ni la wazee na wachezaji wenyewe kwa kutaka ushindi kwa dhana ya kutumia nguvu za kiza. lakini mwalimu hubaki pembeni.

Alisema dhana hiyo ni potofu na hata alishawahi kumwambia mtu mmoja kwamba wanahitaji  utaalamu wa kisayansi kushinda na sio tunguli."Mpira ni training, mkifanya vyema katika hilo mnashinda,".

Vituko
Alisema kwamba  katika maisha yake ya soka ameshuhudia vituko vingi lakini kikubwa ni kile 

kinachohusu wapiganaji wa kijeshi na wenzao wa Polisi: Ugomvi huu wa michezo ulifanya mpaka brigedi kuingia kati kuzima mapigano huko Tabora.

Anachopenda
kwa sasa akafikiria anapenda nini, hakuna sinema, hakuna dansi lakini alisema kwa amani kabisa: 

"Ninapenda ibada, kumtukuza Mungu, baada ya shughuli zangu za mchana , ndiyo kusema napenda ibada" alisema Bakari .
na Beda Msimbe

KATAVI KUZINDUA MKOA NA MATUMAINI MAKUBWA

WAKATI serikali mkoa mpya wa Katavi inajipanga kuzindua mkoa, mkuu wa mkoa huo Dk Rajab Rutenge amesema anaamini kuwa miaka 15 ijayo mkoa huo utakuwa na mchango mkubwa kwa ustawi wa taifa.

Amesema kwamba kinachotakiwa sasa ni kujipanga na kutekeleza mpango mkakati wenye sehemu tano wa kuleta  maendeleo kwa wananchi na kukaribisha wawekezaji.

kauli hiyo ameitoa katika mahojiano maalumu na gazeti hili  ofisini kwake Mpanda.

"Mpango mkakati huu unatekelezeka na unaenda sambamba na mpango wa taifa wa maendeleo" alisema Dk Rutenge na kuongeza kuwa mkoa huo una mpango wa miaka 20 unaotoa dira ya maendeleo.

Alisema japokuwa mkoa huo ambao utazinduliwa katika sherehe maalumu zitakazofanyika kuanzia  19/11 hadi 25 mwaka huu; staili ya uzinduzi umelenga kujitathmini na pia kuonesha wadau wengine fursa mbalimbali za maendeleo na uwekezaji mkoani.

Alisema uzinduzi huo utakaombatana na makongamano na wakazi wa mkoa huo kwa nafasi zao kuonesha nini wanafanya katika kujikwamua kutoka umaskini, utaangalia mafanikio ya kongamano kubwala uwekezaji lililofanyika mwaka jana.

Mkuu wa mkoa alisema wanatarajia viongozi wakuu wa serikali kufungua na kufunga wiki hiyo ya uzinduzi.

Alisema mkoa huo wenye fursa kubwa za uwekezaji katika kilimo cha mazao mbalimbali, na ufugaji utalii,migodi ya madini mbalimbali yenye majina madogo na makubwa umweka kipaumbele chake kuwapatia watu maji, bidhaa ambayo wanatumaini itafungua maeneo mengi ya maendeleo.

Aidha alisema utalii wa ndani na wa nje unatarajiwa kuongezeka hasa kutokana na serikali kuendelea kufungua njia na kuwapo kwa kiwanja cha ndege cha Mpanda.

Mkoa wa Katavi umejaliwa neema ya kuwa na wanyama wengi na wakubwa kutokana na lishe nzuri, maeneo ya matambiko maarufu kwa wenyeji na wakazi wanaokuja kutafuta tiba,chemchem za maji moto,mabaki ya ngome za wakoloni na ziwa lenye samaki wa aina mbalimbali.Aidha ni eneo lenye ufugaji wa nyuki.


UWANJA WA NDEGE MPANDA  KUFUNGUA KATAVI

UWANJA wa Ndege wa Mpanda ambao kwa sasa una njia ya kukimbilia ndege yenye uwezo wa kuchukua hata ndege  aina ya ATR 72 unajipanga kuifikisha njia hiyo kuwa kilomita 3 na kuhudumia mikoa na nchi jirani .

Uwanja huo kwa sasa una njia ya kukimbilia ndege ya kilomita 2.

Taarifa kutoka ofisi ya Mkuu wa MKoa wa Katavi,dk Rajab Rutenge imesema kwamba wanataka kuufikisha uwanja huo katika nafasi ya kuhudumia nchi za maziwa makuu na hasa baada ya kufunguliwa kwa uwanja wa ndege wa kimataifa wa Mbeya.

Uwanja huo ambao kwa sasa unatua ndege za kukodi unafanya mazungumzo na mashirika ya mafuta ili kuweza kutoa huduma za mafuta katika uwanja huo ambazo kwa sasa hazipo.

Hata hivyo tayari ndege za kukodi zinatua katika uwanja huo na kampuni moja ya Mwanza imeanza kutafakari kuwa na safari za mara moja kwa wiki, kwa kutumia ndege ndogo kutoka Mwanza.

Tayari huduma hiyo inayounganisha Mwanza, Tabora na Sumbawanga inatangazwa kwa nguvu mkoani hapa na watu wameambiwa wanaweza kukata tiketi kwa kutumia simu zao.

Kuanza kutumika kwa uwanja huo kwa safari za kibiashara kutafungua zaidi biashara ya utalii katika hifadhi ya taifa ya Katavi na maeneo mengine ya kihistoria kandoni mwa Ziwa Tanganyika.


BUSARA ZA RC ZAONDOA MVUTANO WANAJESHI NA WAFANYABIASHARA

Mzozo kati ya wafanyabiashara wa mahindi na wanajeshi waliopewa jukumu la kusafirisha mahindi kutoka Sumbawanga-Mpanda hadi Shinyanga umetatuliwa na busara za mkuu wa mkoa wa Katavi Dk Rajab Rutengwe na hivyo kuifanya kazi ya usafirishaji mahindi kwenda inavyostahili.

Akizungumza na mwandishi wa habari hizi kuhusu usafirishaji wa mahindi katika njia hiyo alisema kwamba kumekuwepo na mabehewa machache mno ambayo hayawatoshi wanajeshi wala wafanyabiashara wadogo wanaosafirisha bidhaa zao.

"Hivi karibuni ilibidi kutumia busara ili kuleta amani" alisema Mkuu wa mkoa na kuongeza kuwa wakati wanajeshi wanahitaji mabehewa hayo wananchi nao walianza kunung'unika  kwa kutopewa mabehewa na ndipo nilipoagiza kwamba wananchi wapewe mabehewa ili waondoke mara moja na safari inayofuata iwe ya kampeni ya wanajeshi.

Alisema hali hiyo ilileta nafuu kwani hata kama mabehewa 21 yaliyofika wangeligawana, wanajeshi yasingeliwatosha na wananchi nao wasingeliwatosha na kutoridhika kuendelea na hivyo kuleta mgongano wa kimaslahi.

Alisema ipo haja ya kuimarisha uletaji wa mabehewa ili kampeni ya kusafirisha mahindi  yote kutoka Sumbawanga na Mpanda iweze kukamilika mapema.

kwa zaidi ya miezi miwili wanajeshi wanahamisha mahindi kutoka sumbawanga hadi Mpanda na kuyapeleka kwenye maghala ya Shinyanga lakini uhaba wa mabehewa unaonekana kuwapunguza kasi yao.

Jumatatu wiki hii Katibu Mkuu Ulinzi alifika mkoani hapa katika ziara ya kukagua maendeleo ya kampeni hiyo ya kuokoa mahindi kabla ya mvua kuanza.

Aidha naibu katibu Mkuu wizara ya Kilimo,chakula na ushirika Mbogo Mfuta kamba naye alikuwa katika ziara ya mikoa ya Rukwa na katavi kujionea jinsi operesheni hiyo inavyoendelea na kuweka mikakati ya kuongeza kasi katika kilimo.

Mikoa ya Katavi na Rukwa ni miongoni mwa mikoa inayotegemewa kama ghala la nafaka kwa Tanzania.

KARAKANA YA WALEMAVU YAPELEA 

KARAKANA  ya walemavu inayojengwa kuanzia mwaka 2008 mjini Mpanda imepelea na kufanya mradi mzima wa kuwawezesha walemavu kujitegemea kwa kupewa elimu ya ufundi kuchelewa kuanza.

Katibu wa chama cha walemavu Mpanda, Godfrey sadalla amesema kwamba kuchelewa kumalizika kwa jengo walilolianza mwaka huo zinafanya juhudi za kumkomboa mlevu kukwama.

Mradi huo ambapo mpaka utakapokamilia utakuwa  ni shilingi milioni 49.8 ulipigwa jeki na TASAF kwa shilingi milioni 9 na sasa upo katika rinta wakati SIDO walitoa baadhi ya zana zinazotakiwa kuwepo katika karakana kama cherahani na vifaa vya kutengenezea viatu.

Sadalla alisema kwamba ili kukamilisha wanahitaji shilingi milioni 24 ambazo zlisema wakati wa mwenge Mkurugenzi wa Halmashauri aliwahidi kuwachangia.

Alisema mradi huo wa karakana ambao ulitarajiwa kutoa mafunzo ya ushonaji,ufundi wa kuunga vyuma,ufundi wa viatu na ufundi seremala unamilikiwa na kikundi cha walemavu chenye wanachama 49.

Alisema walemavu ni watu wa kawiada ambao wakipata elimu na utaalamu wa kutosha wataondokana na kuwa mzigo kwa familia na hata kwa taifa.

"hatutaki kuomba, mradi huu unataka kusaidia walemavu wote kupata ujuzi na kujiajiri we nyewe au katika vikundi" alisema Sadalla ambaye kitaaluma ni fundi viatu.
Alisema ufundi huo alijifunzia chuo cha walemavu Yombo.
pamoja na kuelezea mradi huo mkubwa alisema kwamba wangelipenda kuwa na watu wa kujitolea wa kuweza kuwafunza ili wawe na utaratibu wa maisha kama wenzao wa mikoa ya kaskazini ambako watu wa kujitolea wamefanya kazi kubwa ya kufundisha na kuwaaminisha walemavu.

Hata hivyo alisema kama taasisi mbalimbali zitawakumbuka na kukamilisha jengo lao wanahakika kampeni yao ya kutaka wazazi wenye watoto walemavu wasifungie watoto wao majumbani itafanikiwa.

 KATAVI SIASA KUTOKWAMISHA MAENDELEO-RC
 Na Beda Msimbe
MKOA wa Katavi umefanikiwa kukuza mahusiano kati ya serikali,Chama tawala na wapinzani na hivyo kuongeza kasi ya kusaka maendeleo miongoni mwa wananchi wake.
Kauli hiyo imetolewa na mkuu wa mkoa wa Katavi Dk Rajabu Rutengwe katika mahojiano na gazeti hili kuhusu hali ya kisiasa ilivyo kwa sasa mkoani humo.
Alisema ingawa miaka miwili iliyopita hata kabla ya kuanza kwa mkoa mpya hali ya msuguano ilikuwa tete,kwa sasa hali hiyo haipo na kwamba wananchi wanaanza kuelewa umuhimu wa kusukuma mbele kazi za ujenzi wa taifa.
Msuguano mkubwa ulikuwa kati ya mashabiki wa Chadema na mamlaka  mbalimbali za serikali na chama tawala hasa katika masuala ya maendeleo.Katavi unaweza kusema kwamba ni ngome ya Chadema.
Dk Rutengwe alisema Kwamba serikali ya mkoa ilifanyakazi kubwa ya kuondoa na kudhibiti mawazo hasi ya kimaendeleo ambayo yalikuwa yanakwamisha.
"Maendeleo yataletwa na wanakatavi wenyewe;kubuni,kupanga, kutekeleza mipango yenyewe inawezekana tu kwa kuwa na utashi usiozingatia itikadi bali hoja muhimu ya maendeleo" alisema Mkuu wa mkoa na kuongeza kuwa wananchi wa Katavi kwa sasa wanatambua kwamba kuna umuhimu wa kuhimizana maendeleo.
Mkuu wa mkoa alisisitiza kwamba mkoa wake una dira tayari ya maendeleo ya miaka 20, dira ambayo inawaelekeza wanakatavi namna gani waende na kuweka maeneo yao katika hali tayari kuchangia uchumi binafsi wilaya,mkoa hadi taifani.
Kwa mujibu wa mkuu wa mkoa mpango huo umegawanyika kati ya muda mrefu na muda mfupi.Mipango ya muda mrefu pamoja na mambo mengine imelenga kuiwezesha Mpanda kupata hadhi ya manispaa
Hata hivyo mkuu huyo wa mkoa amesema kwamba bado zipo changamoto kadhaa ambazo zinaweza kabisa kusaidia watu kupingana bila jazba bali kwa hoja  kwa ajili ya maendeleo.
MATAMBIKO KUREJESHA UHAI NA USALAMA WA KATAVI
 KUREJESHWA kwa shughuli za matambiko katika hifadhi ya taifa ya Katavi kumeelezwa kufanikisha malengo ya ruhusa hiyo, ya kuweka salama hifadhi na kuipa uendelevu.
Hayo yalielezwa na Mhifadhi wa katavi Davis Mushi wakati akielezea sababu za kurejeshwa kwa matambiko katika hifadhi ya Katavi kiasi cha miaka miwili iliyopita.
Alisema hoja ya kurejesha ruksa hiyo inaonesha matunda kwani kumekuwepo na ushiriki wa moja kwa moja wa kulinda maeneo ya Matambiko yaliyoko hifadhini na hivyo kuilinda hifadhi dhidi ya mioto na uwindaji haramu.
"Ndugu mwandishi  wazee hawa wanapofanya matambiko katika maeneo yao, wakirejea nyumbani wanaelezea umuhimu wa mizimu inayotambikiwa kuishi kwa amani na kutoharibiwa kwa mazingira yake na hilo ndilo Hifadhi ya Katavi inalitamani." alisema Mushi na kuongeza kuwa sauti ya wazee husikika zaidi na hivyo kupitia kwao hifadhi itaendelea kuwepo
Katika mbuga ya Katavi kuna maeneo takribani manne yanayofanyiwa matambiko likiwemo eneo la mzimu wa Katabi mwenye kuleta asili ya katavi.Mzimu huo unaelezwa kuwa ni mali ya Wadembe na wapimbwe.
Mzimu huo unaowakilishwa na  miti mikubwa miwili upo kandoni mwa ziwa Katav na inasemekana hufanya maajabu mbalimbali.
Kwa mujibu wa Mushi tayari we nye matambiko katika hifadhi wameshafanya matambiko hayo huku wao wakitoa askari kwa ajili ya usalama wao ili wasivamiwe na wanyama wakali. 
VIJANA WATAKA HUDUMA KARIBU NAO
 VIJANA wa Usevya wilayani Mlele mkoani Katavi wameitaka serikali kusogeza huduma za elimu na ufundi kwa vijana walioko maeneo ya pembezoni ili kuwezesha vijana hao kupata maarifa mapya kukabiliana na changamoto za ajira.
 Wakizungumza na mwandishi wa habari hizi hivi karibuni vijana hao wamesema kwamba kjuhudi hizo zisipofanyika vijana wanakuwa na mawazo mgando kuhusu ajira na hivyo kuwa bomu la kitaifa. 
"Tuna matatizo mengi sana lakini moja linalokera ni ukosefu wa ajira. Kilimo kipo lakini hakuna msukumo na vijana wanajibweteka tu " alisema Antony Mhanda ambaye hata hivyo alimshukuru Waziri Mkuu Mizengo Pinda kwa kuwapatia trekta kubwa kubadili namna ya kuendesha kilimo katika eneo hilo.
Walisema vijana hawana elimu ya kutosha katika mambo mengi kuanzia siasa,elimu ya demokrasia,afya ya uzazi kutokana na kuwa katika ukanda ambao hauna vyombo vya mawasiliano redio wala magazeti.
"Kutokana na ukosefu wa elimu kuna tatizo la mimba za utotoni japo zimepungua. Kondomu zipo lakini elimu ya afya ya uzazi ni kidogo" alisema Sebastian Beshumsi katika mazungumzo hayo.
Vijana hao wamesema wanapokuwa hawakuchaguliwa kuendelea na elimu ya msingi hawana mahali pengine pa kujiendeleza hasa ukizingatia umbali uliopo na maeneo yenye kuendesha elimu hiyo mkoani Katavi.
 Alisema kukosekana kwa elimu hata masuala ya ujasiriamali hayajadiliwi, kwani hata hawajui fursa zilizopo katika kujiendeleza na kama ni suala la mikopo nini kifanyike.  Usevya ipo kiasi cha kilomita  nane kutoka eneo la Kibaoni ambako ndiko nyumbani kwa waziri Mkuu Pinda.Aidha wapo takariani kilomita 150 kutoka Mpanda mjini. 
"waliofika mjini wanazungumzia usafiri wa pikipiki, tunauhitaji san ahuku kutokana na umbali wa maeneo yetu, lakini unajifunza wapi kuendesha pikipiki, unapata wapi fedha za kununulia pikipiki?" alisema Mhanda na kuomba serikali kuwasogezea elimu.
MVUA KUSITISHA UJENZI WA KIGAWA MAJI KAREMA
 UJENZI wa Kigawa maji  katika bonde la Nkuswe, Karema kwenye skimu ya umwagiliaji ya Karema utasitishwa mara tu masika itakapoanza.
Kusitishwa kwa ujenzi huo kunamaananisha kwamba mradi huo huenda ukakamilika Juni mwakani.
 Awali kigawa maji hicho  kilitarajiwa kumalizika Desemba mwaka huu.
"Mvua zikianza hapa  bonde lote hili hufurika, hatuwezi kuendelea na kazi" alisema mtunza ghala aliyekuwa eneo la ujenzi Jerome Paul.
Alisema japokuwa mto huo si endelevu, wakati wa masika hleta kizaazaa kikubwa na kw amujibu wa takwimu walizonazo hawawezi kuendelea na ujenzi huo katika kipindi hicho.
 Alisema katika mauzngumzo klwamba kwa sasa wanajenga gkala ndogo na ofisi kwa ajili ya kuhjifadhi taarifa zao na zana zao wakati utakapofika.
 Kwa kawaida masika katika mkoa wa Katavi huanza mwishoni mwa mwezi wa Kumi au mwanzoni mwa mwezi Novemba na mvua zake huwa nyingi kutokana na mkoa kuwa bado na misitu mingi.
 Kigawa maji hicho kinategemewa kukuza kilimo katika skimu ya Karema yenye wakulima wadogo wadogo.
 WAKONONGO WATAMBIKIA AMANI
 WATU wa kabila la wakonongo wanaopatikana katika mkoa wa Katavi, wilaya ya Mlele hufanya matambiko makubwa mara mbili kwa mwaka na ya dharura kila mwezi kwa lengo la kuombea amani na uchumi.
Chifu Kayamba ll akizungumza kutoka katika makazi yake yaliyopo Iyonga, alisema amani ikipotea masahihisho yake ni magumu ndio maana wao kila mwezi wanafanya tambiko la kuombea amani kwenye taifa.
Alisema kiongozi mwenye busara ni yuile ambaye atawezesha amani kwani kupitia maani shughuli nyingine za kujiletea kipato na maendeleo kinawezekana.
Aidha alisisitiza kwamba hakuna kitu kisichokuwa na mila; mwanzo wa jambo lolote ni mila na kusikitika namna wananchi wanavyoacha mila zao na kuzikumbatia za kigeni ambazo nyingi ni kasumba kwa ajili ya kuwezesha kutawaliwa kwa wananchi na kutawala kwa upande wa wakoloni.
Alisema sehemu kubwa ya matatizo yaliyopo nchini yanaweza kuondolewa kwa kuzingatia mila ambazo zinatoa mamlaka kwa wasimamizi kuhakikisha kuna maendeleo, amani na upendo.
"Pamoja na kwamba kuna asilimia 80 ya watu vijijini bado wakuu wa kimila hawaheshimiwi na matokeo yake kububujika kwa maadili na kuvurugika kwa tabia nchi. 
Alisema suala la demokrasia limelemaza watu na tafsiri potofu waliyonayo, inawafanya watu kukurupikia hata mambo ambayo hayana thamani kwao huku yakiwagombanisha na wazee wao waliokufa (MIZIMU) ambao wanataka kuwasaidia katika shida mbalimbali.
 Chifu Kayamba ll alisema mila ni mpango wa Mungu na kila anayefuata mila hufanikiwa na ndio mmaana ili sisi (wananchi) tusifanikiwe wakoloni walipiga vita imani za wenyeji.