Friday, May 17, 2013

VODACOM PREMIER LEAGUE

May 17, 2013

PAZIA LIGI KUU YA VODACOM KUFUNGWA JUMAMOSI TFF LEO


Ligi Kuu ya Vodacom (VPL) kuwania ubingwa wa Tanzania Bara msimu huu (2012/2013) inafikia tamati kesho (Mei 18 mwaka huu) kwa timu zote 14 kupambana katika viwanja saba tofauti.  

Mechi zote zitachezwa kuanzia saa 10 kamili jioni. Ni jukumu la kamishna wa mechi husika kuhakikisha mchezo unaanza katika muda uliopangwa, vinginevyo hatua za kinidhamu zitachukuliwa kwa mujibu wa Kanuni za Ligi Kuu ya Vodacom toleo la 2012.
Yanga ambayo tayari imeshatwaa ubingwa itakuwa mgeni wa Simba katika mechi namba 180 itakayochezwa Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam ambapo mwamuzi atakuwa Martin Saanya kutoka Morogoro na Kamishna ni Emmanuel Kavenga wa Mbeya.

Mgambo Shooting vs African Lyon (Uwanja wa Mkwakwani, Tanga. Mwamuzi ni Amon Paul wa Mara wakati Kamishna ni Ally Mkomwa kutoka Pwani), JKT Ruvu vs Mtibwa Sugar (Uwanja wa Azam Chamazi, Dar es Salaam. Mwamuzi ni Israel Mujuni wa Dar es Salaam wakati Kamishna ni Salum Kikwamba kutoka Kilimanjaro).

Tanzania Prisons vs Kagera Sugar (Uwanja wa Sokoine, Mbeya. Mwamuzi ni Ibrahim Kidiwa wa Tanga wakati Kamishna ni John Kiteve kutoka Iringa), Oljoro JKT vs Azam (Uwanja wa Sheikh Kaluta Amri Abeid, Arusha. Mwamuzi ni Athuman Lazi wa Morogoro wakati Kamishna ni Juma Mgunda kutoka Tanga).

Uwanja wa Jamhuri, mjini Morogoro utatumika kwa mechi kati ya Polisi Morogoro na Coastal Union ya Tanga ambapo Mwamuzi atakuwa Said Ndege wa Dar es Salaam wakati Kamishna ni Hakim Byemba kutoka Dodoma. Toto Africans itacheza na Ruvu Shooting katika Uwanja wa CCM Kirumba jijini Mwanza ambapo mwamuzi ni Geoffrey Tumaini kutoka Dar es Salaam na Kamishna ni Josephat Magazi wa Singida.

 MECHI ZA MARUDIANO RCL WIKIENDI HII

Mechi za marudiano za raundi ya kwanza ya Ligi ya Mabingwa wa Mikoa (RCL) zinachezwa wikiendi hii katika viwanja kumi tofauti wakati mechi ya Flamingo ya Arusha na Machava FC ya Kilimanjaro yenyewe itachezwa Jumatatu (Mei 20 mwaka huu).

Uamuzi wa mechi hiyo kuchezwa Jumatatu ni kutokana na Uwanja wa Sheikh Kaluta Amri Abeid kutumika kwa mechi ya Ligi Kuu ya Vodacom (VPL) kesho wakati Jumapili utatumika kwa shughuli nyingine za kijamii kwa mujibu wa wamiliki wa uwanja huo (CCM Mkoa wa Arusha).

 Mechi nyingine zitachezwa keshokutwa (Jumapili) ambapo Abajalo watakuwa wenyeji wa Red Coast kwenye Uwanja wa Kumbukumbu ya Karume, Dar es Salaam. Uwanja wa Nangwanda Sijaona mjini Mtwara utatumika kwa mechi kati ya wenyeji Coast United na Kariakoo ya Lindi.

 African Sports ya Tanga itaoneshana kazi na Techfort ya Ifakara mkoani Morogoro katika mchezo utakaochezwa Uwanja wa Mkwakwani. Nayo Simiyu United ya Simiyu itakuwa mgeni wa Magic Pressure ya Singida kwenye Uwanja wa Namfua, mjini Singida.

 Uwanja wa CCM Kirumba jijini Mwanza ndiyo utakaotumika kuzikutanisha timu za Polisi Jamii Bunda kutoka Mara na wenyeji UDC wakati Biharamulo FC ya Kagera na Polisi SC ya Geita zitaumana kwenye Uwanja wa Kaitaba mjini Bukoba. 

Milambo FC ya Tabora itakuwa mwenyeji wa Saigon FC ya Kigoma kwenye Uwanja wa Ali Hassan Mwinyi mjini Tabora huku Mbinga United ya Ruvuma ikiikaribisha Njombe Mji ya Njombe kwenye Uwanja wa Majimaji mjini Songea.

Uwanja wa Kumbukumbu ya Samora mjini Iringa utatumika kwa mechi kati ya wenyeji 841 KJ dhidi ya Kimondo SC kutoka Mbeya. Nazo Rukwa United na Katavi Warriors zitapimana ubavu kwenye Uwanja wa Nelson Mandela mjini Sumbawanga.

 Timu zitakazofuzu kucheza raundi ya pili zitacheza mechi zao za kwanza kati ya Mei 25 na 26 mwaka huu wakati mechi za marudiano ni kati ya Juni 1 na 2 mwaka huu.

 UTARATIBU WA SAFARI MECHI YA TAIFA STARS v MOROCCO

Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) litasaidia upatikanaji wa visa kwa waandishi wa habari na Watanzania wengine wanaotaka kwenda Morocco kushuhudia mechi kati ya Taifa Stars na Morocco itakayochezwa Juni 8 mwaka huu jijini Marrakech, Morocco.

Kwa ambao wangependa kupata visa kupitia TFF wanatakiwa kuwasilisha pasipoti zao, ada ya visa ambayo ni dola 50 za Marekani pamoja na picha mbili zenye kivuli (background) ya rangi nyeupe kabla ya saa 6 kamili Mei 20 mwaka huu.

 Boniface Wambura Mgoyo

Ofisa Habari

Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF)
 

MAMA TUNU PINDA AWAASA MAKATIBU MUHTASI WAZINGATIE MAADILI YA KAZI YAO


mama pinda 5 
MKE wa Waziri Mkuu, Mama Tunu Pinda amewataka Makatibu Muhtasi kuzingatia maadili ya taaluma yao ya uhazili ili kuongeza ufanisi wa majukumu ya kazi zao.
 
Ametoa wito huo jana  Mei 16, 2013 wakati akifungua Kongamano la Tatu la Makatibu Muhtasi (Tanzania Personal Secretaries Association – TAPSEA) kwenye ukumbi wa Mikutano wa Kimataifa jijini Arusha (AICC).
 
Kongamano hilo la siku mbili, limehudhuriwa na Makatibu Muhtasi zaidi ya 1,500 kutoka mikoa yote nchini, na baadhi ya wawezeshaji kutoka Kenya, Uganda na Rwanda.
 
Mama Pinda alisema umuhimu wa taaluma ya uhazili katika tasisi ni mkubwa sana na siyo kitu cha kubeza hata kidogo
Umuhimu wa taaluma ya uhazili katika taasisi tunazofanyia kazi unatokana na nafasi  kubwa ya makatibu muhtasi kama wasimamizi wa ofisi na wasaidizi wa watendaji wakuu. Nafasi yenu inawapa fursa ya kuandaa na kutunza nyaraka mbalimbali za kiofisi zinazohusu menejimenti ya taasisi hizo. Niwaombe makatibu muhtasi wote mzingatie maadili ya kazi ya uhazili katika kutekeleza majukumu yenu,” alisisitiza.
 
Aliwataka waongeze jitihada za kukiimarisha Chama chao ili hatimaye TAPSEA iweze kuenea Mikoa yote na kuwa Chombo kitakachosimamia miiko na maadili ya fani ya Uhazili kama zilivyo taaluma zingine nchini.
 
Alisema majukumu ya makatibu muhtasi siyo kupiga chapa pekee na kuongeza kwamba, kama chama cha kitaaluma, TAPSEA lazima iendeleze jitihada za kubadili mtazamo huo ili jamii iweze kutambua umuhimu wa nafasi ya makatibu muhtasi katika taasisi mbalimbali za umma na za sekta binafsi.
 
“Hata hivyo, napenda ieleweke kwamba kazi ya kuleta mabadiliko ya kimtazamo inaanzia kwa katibu muhtasi mwenyewe. Nawashauri wanachama wote wa TAPSEA wawe mstari wa mbele katika kubadilika kifikra na kujiendeleza kila wakati ili kujijengea uwezo wa kuzikabili ipasavyo changamoto za taaluma ya uhazili katika mazingira ya sasa,” alisema.
 
Mama Tunu Pinda alisema kuwekeza katika teknolojia ni jambo muhimu lakini teknolojia pekee haiwezi kuleta mabadiliko chanya katika kuboresha huduma na kuongeza tija hivyo teknolojia ni lazima iende sambamba na uwekezaji katika rasilimali watu kwa watumishi kusoma zaidi na kupatiwa fursa za mafunzo zaidi ndani na nje ya nchi
 
Mama Tunu Pinda ambaye alikuwa mgeni rasmi katika kuzindua kongamano hilo pia alizindua TAPSEA SACCOS na kuwataka makatibu muhtasi hao wajiunge kwa wingi ili kutunisha mfuko wa SACCOS hiyo.
 
Mapema, akimkaribisha kuzungumza na washiriki wa mkutano, Mlezi wa TAPSEA Dk. Mary Nagu ambaye pia ni Waziri wa Nchi, Uwekezaji na Uwezeshaji aliwataka wawe waaminifu katika kuijenga TAPSEA SACCOS ili hatimaye ifikie hatua ya kuwa benki yao maalum kama ilivyo kwa Chama cha Walimu nchini.
 
Mshauri wa Kisheria wa TAPSEA, Naibu Waziri wa Katiba na Sheria, Bi. Angela Kairuki aliwataka washiriki wa kongamano hilo kuzingatia maadili kwa kutunza siri za ofisi wanazozitumikia.
 
“Inasikitisha kuona kila mara kunakuwa na taarifa ambazo zinavuja lakini ukifuatilia wapi taarifa hizo zimetokea utabaini kuwa chanzo ni makatibu muhtasi… ninawaomba sana mjitahidi kutunza siri za taasisi zenu,” alisisitiza.